Dar es Salaam. Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwele amezindua ghati namba moja katika Bandari ya Dar es Salaam itakayoongeza uwezo kupokea kontena za mizigo.
Akizungumza leo jioni Jumanne Juni 11, 2019 Kamwelwe amesema kabla ya ghati hiyo kuwepo, walikuwa wakipokea kontena 2, 000 hadi 2,800.
Amesema baada ya kuanza kazi kwa ghati hiyo yenye urefu wa mita 191, uwezo wa kupokea kontena za mizigo utakuwa kati ya kontena 4,000 hadi 6,000.
"Kutakuwa na uwezo wa meli kubwa kuingia, nimewaagiza TPA (Mamlaka ya Bandari Tanzania) warahakishe vifaa kwa ajili ya kupakulia mizigo kwa sababu ufanisi hauwezi kuwepo tena," amesema Kamwelwe.
Kwa mujibu wa TPA, ghati hiyo iliyokamilika ujenzi wake Novemba, 2018 ni sehemu ya ghati nane zitakazojengwa kwa Sh968bilioni za mkopo wa Benki ya Maendeleo ya Uingereza.