UMOJA wa Ulaya (EU) umeipatia Tanzania Sh bilioni 27 kwa ajili ya kuongeza mnyororo wa thamani wa uzalishaji mazao ya nyuki kwa ajili ya kuwanufaisha wafugaji wa nyuki nchini.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Dk Batilda Buriani alitoa kauli hiyo jana wilayani Uyui wakati wa ziara yake ya kukagua shughuli za maendeleo na kutembelea msitu wa Karangasi ambao wananchi wameanza kuufyeka ili kulima korosho.
Alisema kwamba mradi huo utatekelezwa katika mikoa ya Tabora, Kigoma, Singida, Katavi, Shinyanga na maeneo ya Kisiwa cha Pemba.
Batilda alisema katika mradi huo utawawezesha wafugaji kuongeza mnyororo wa thamani wa uzalishaji wa mazao ya nyuki kupitia mizinga ya kisasa na kuongeza utaalamu katika ufugaji.
“Serikali imeamua kuleta miradi mbalimbali ikiwemo wa kuongeza mnyororo wa thamani kwenye mazao ya nyuki ili kuwaondoa katika umaskini wafugaji wa nyuki,” alisema.
Mratibu wa Mradi wa Kuongeza thamani ya mazao ya nyuki, Magdalena Muya alisema kuwa mradi huo utatekelezwa katika kipindi cha miaka sita nchini.
Alisema Umoja wa Ulaya umeamua kuleta mradi huo baada ya kufuatilia na kubaini kuwa asali inayoingizwa nchini mwao haitoki katika nchi jirani bali Tanzania na hasa mikoa yenye miti ya miombo.