WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Ummy Mwalimu, amelitaka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kutokuwa kikwazo kwa namna yoyote, kwa wawekezaji nchini.
Akizungumza na Menejimenti ya NEMC jijini Dar es Salaam, Waziri Ummy alilitaka pia NEMC kuimarisha ofisi zake za kanda na kuwajengea uwezo wafanyakazi ili wamudu kasi ya uwekezaji na kuondoa mrundikano wa mambo katika ofisi za makao makuu ya baraza hilo.
Alisema uchumi wa viwanda utafikiwa kwa kuwekwa mazingira mazuri yatakayovutia wawekezaji na kwamba, suala hilo linahitaji mikakati mizuri.
Aidha, alilitaka baraza hilo kuwashauri wawekezaji kwani baadhi ya wataalamu elekezi si waaminifu kwa kuwa wamekuwa wakirefusha mchakato wa upatikanaji wa huduma kwa wawekezaji zikiwemo za utoaji wa vibali hali inayolitia doa NEMC.
Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dk Samuel Gwamaka, alisema
baraza hilo limejipanga kutekeleza na kusimamia miradi yote ya kimkakati kwa ufanisi na sasa baada ya maelekezo ya waziri, itakuwa rahisi kutekeleza mipango yake.