Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amezindua programu ya ‘Kopa Ngo’mbe Lipa Maziwa’ yenye lengo la kuwainua kiuchumi vijana na wanawake kupitia shughuli za ufugaji.
Ulega amezindua programu hiyo katika hafla ya kukabidhi Ng’ombe 300 kwa Kampuni ya Kahama Fresh ambao watakopesha vijana na Wanawake waweze kujikwamua kiuchumi kupitia uzalishaji wa maziwa.
“Kwa dhati napenda kuipongeza kampuni ya Kahama Fresh kwa kutekeleza Programu ya Kopa Ng’ombe Lipa Maziwa inayolenga kukiwezesha kiwanda cha Maziwa cha Kahama Fresh kupata malighafi lakini pia kuwawezesha wafugaji wa Karagwe kuongeza uzalishaji wa maziwa na hivyo kujikwamua kiuchumi”, alisema Ulega
Waziri Ulega ameipongeza Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania – TADB kwa kutoa mkopo kwa kampuni ya Kahama Fresh ili iweze kununua mitamba bora 600 kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa maziwa na kuimarisha uwekezaji wa Mtanzania mzawa ambaye amewekeza kwa jamii kupitia Mifugo.