NAIBU Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega, amewaagiza viongozi wa viwanda vya kuchakata samaki mkoani Mwanza kukaa na maofisa kutoka katika wizara hiyo kutafuta suluhu ya ukosefu wa samaki wa kutosha katika viwanda vyao ili viweze kufanya kazi kadri inatarajiwa.
Ulega amesema hayo leo alipotembelea viwanda vya kuchakata minofu ya samaki vya Tanzania Fish Processor na Victoria Perch Limited baada ya kupata malalamiko kutoka kwa baadhi ya viongozi wa viwanda juu ya ukosefu wa malighafi ya samaki aina ya sangara na kuathiri shughuli za uzalishaji.
Akitoa maelekezo, Ulega amesema ukosefu wa malighafi unadaiwa kupungua viwandani kutokana na vitendo vya uvuvi haramu, biashara ya mabondo na bei ndogo ya samaki wanaonunuliwa katika viwanda hivyo na kuelekeza viongozi wa viwanda na maafisa kutoka wizarani kukaa pamoja na kubaini kiini hasa cha tatizo hilo ili kutafuta suluhu.
“Sisi tunafurahi tukisikia wananchi wanapata, wakati huo tunataka viwanda vipate malighafi yote mawili tunayataka lazima tuwe na nyongeza ya maarifa ili tupate suluhu ya jambo hili tutoke kwa mafanikio wote wafurahi,” alisema.
Alisema uwepo wa viwanda vya kuchakata samaki unalinufaisha taifa kwa kuwa serikali inapata mrabaha wa mazao yanayoenda nje ya nchi ambapo fedha hizo zinatumika katika shughuli mbalimbali zikiwemo za kijamii.
Kuhusu kudhibiti vitendo vya uvuvi haramu amesema wizara imejipanga vyema na kuwataka watu wote wanaojishughulisha na vitendo hivyo kuacha mara moja na kwamba serikali itaongeza juhudi za kupambana na uvuvi haramu na kutaka ushirikiano kutoka kwa kila mdau.