Wakazi wa Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi mkoani Morogoro, watapata huduma bora ya umeme na ya uhakika baada ya kukamilika ujenzi wa mradi mkubwa wa kituo cha kupooza na kusambaza umeme Ifakara kitakachokuwa na uwezo wa kuzalisha Megavolt 20 (MVA 20 ), ifikapo Agosti mwaka huu.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy amesema hayo Mei 5,2023 mjini Ifakara wakati wa ziara ya wabia wa maendeleo wa mradi huo wakiongozwa na Umoja wa Ulaya.
Mhandisi Saidy amesema mradi huo mkubwa unagharamiwa na Serikali ya Tanzania kwa Ushirikiano na Umoja wa Ulaya na umetengewa kiasi cha zaidi ya Sh bilioni 22.8 na ujenzi wake hadi sasa umefikia asilimia 90.