Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania na Uganda zimekubaliana kuunda timu maalumu katika Wizara za Mambo ya Nje itakayokuwa na jukumu la kufuatilia makubaliano yanayofikiwa kwenye Tume ya Pamoja ya Kudumu (JPC) na kusimamia utekelezaji wake.
Hayo yamebainishwa leo Ijumaa Septemba 6, 2019 jijini Dar es Salaam na mawaziri wa mambo ya nje wa nchi hizo, Profesa Palamagamba Kabudi wa Tanzania na Sam Kutesa wa Uganda katika kongamano la biashara kati ya Tanzania na Uganda.
Katika kongamano hilo, nchi hizo zimetiliana saini makubaliano katika maeneo matatu ambayo ni uendelezaji wa sekta ya kilimo, uhamiaji na magereza na kikao cha tatu cha Tume ya Pamoja ya Kudumu.
Akizungumza kwenye kongamano hilo mbele ya marais wa nchi hizo, John Magufuli na Yoweri Museven, Kutesa amesema kumekuwa na pengo kubwa katika utekelezaji wa maazimiuo yanayofikiwa kwenye mikutano ya Tume ya Pamoja ya Kudumu (JPC)
Amesema wataongeza mikutano ya mara kwa mara kati ya JPC na sekta binafsi, sambamba na kuwa na timu maalumu kwa ajili ya utekelezaji wa maazimio yanayofikiwa kwenye vikao vya Tume hiyo.
“Ufuatiliaji wa maazimio na utekelezaji wake vimekosekana kwenye mikutano hii. Sasa tumekubaliana kuwa na timu maalumu ambayo itahakikisha kuna utekelezaji baada ya vikao hivyo,” amesema Kutesa.
Pia Soma
- Waziri wa zamani alalamikia bungeni wizi wa vifurushi vya simu
- Hizi ndiyo shahada saba alizosoma Rais Mugabe
Pia, amesema walikubaliana kutiliana saini mikataba ya ushirikiano katika sekta ya kilimo, uhamiaji na magereza.
Amewataka wafanyabiashara kuzitumia fursa zinazopatikana kwenye hizo hizo kwa maendeleo yao.
“Fursa za kibiashara za Tanzania na Uganda ziko nyingi sana. Huu ndiyo wakati wa kuzitumia fursa hizo, tunawashukuru viongozi wetu (Magufuli na Museveni) kwa ushirikiano mnaotupatia,” amesema Waziri Kabudi.