MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), imesema inawafuatilia kwa ukaribu watoa huduma ya nishati ya mafuta ili kuhakikisha vigezo na masharti vinazingatiwa.
Meneja wa Mawasiliano wa EWURA, Titus Kaguo amesema wakati wa Maonesho ya 45 ya Kimataifa ya Biashara yanayofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere Sabasaba jijini Dar es Salaam kwamba "Tumekuwa tunafatilia kwa ukaribu watoa huduma wa nishati ya Mafuta na wanaokiuka kwa kupandisha bei wanachukuliwa hatua pamoja na kufutiwa leseni za utoaji huduma."
Amesema EWURA wanapopanga bei elekezi wanakuwa wameshajiridhisha katika soko la ndani bila kumuathiri muuzaji wa jumla pamoja na yule wa Kati kwenda kwa watumiaji wa Nishati hiyo.
Aidha amesema pasipo kuwepo na udhibiti kungekuwa na mfumuko wa bei na kufanya maisha kupanda kutokana na asilimia 95 inategemea nishati hiyo.