Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Tofauti ya ukapa na ukufuli ni mfumuko wa bei kwa wananchi

18086 Pic+mfumuko TanzaniaWeb

Wed, 19 Sep 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Juhudi zote zilizopita zimezidiwa na juhudi hizi za sasa, kiasi cha kuungwa mkono kuliko zote. Wenye juhudi mbadala wanafungasha virago huko waliko kwenye vyama vyao vya juhudi takataka na kujiunga na juhudi safi.

Juhudi hizi ndiyo pekee ambazo wafanyakazi mwaka wa tatu huu wanapandishiwa mishahara? Vijana wakimaliza tu vyuo wanakutana na ajira, na ajira zimetapakaa mitaani mpaka zingine zinachacha mitaroni? Au nakosea?

Wajanja wote wanaunga mkono juhudi. Sasa wewe endelea kubaki huko uliko. Utajikuta Tanzania nzima imekutenga, watu wako kwenye juhudi wewe ukisubiri huruma za posho za tripu na semina kama ndezi pori.

Imegundulika kuwa watu hawahami kwa hiari yao bali wanashawishiwa na juhudi. Ukitaka maisha bora au cheo kikubwa cha ghafla bin vuu, wewe unga juhudi iwe kwa kamba au gundi utajua wewe na Mungu wako.

Mimi siwezi kutoa jibu lolote kwa janga hili la kuhama kwenye juhudi na kujiunga na juhudi. Ili upate jibu sahihi na wewe zidisha juhudi ya kujiuliza au kujadili na wenzako kuliko kuponda ponda tu.

Kuna mpuuzi mmoja ambaye simuamini hata akinisalimia, eti anadai juhudi ni mpango wa kubadilisha maneno ya kitabu kitakatifu cha taifa, ili huko mbeleni wawaandae waunga juhudi wengi wa kuunga mkono juhudi zao.

Siyo tu kubadilisha maneno na kutupatia maneno mazuri zaidi, eti pia kuweka neno sahihi la mwenye juhudi abaki na juhudi zake milele amina. Ili aendelee kuungwa mkono kwa juhudi zake bila kushindanishwa na mwenye juhudi mwingine.

Akaendelea kuongea uongo wake kuwa wanatuandaa kisaikolojia huko mbeleni waungaji wa juhudi kutoka kwenye juhudi mbadala wapatikane wachache ikiwezekana Mungu akiwapenda zaidi wasiwepo kabisa ili awe mmoja tu.

Waungaji juhudi

Niliendelea kusikiliza uongo wake sikutaka kumuangusha, eti anadai waunga juhudi wanatutoa kwenye njia tusiende kupiga kura, maana hatutakuwa na imani na wenye juhudi mbadala, kwa hisia kuwa wataondoka tena kwenda kuunga juhudi za yuleyule.

Kuna watu waongo na huyu ni mmoja wapo. Ananiambia eti wanaoungwa juhudi hawataki vikundi vya wenye juhudi mbadala. Kwamba hata vikiwepo basi viwe ni vile vyenye kuendeshwa na wao. Lakini wenye vikundi juhudi mbadala halisi watawafuta wote.

Eti wajiandae kutowaona wenye juhudi machachari kutoka katika vikundi mbadala vya juhudi, maana wenye juhudi zao hawataki ushindani. Kama kuna mwenye juhudi mbadala wa kuingia mjengoni basi ni yule asiye na madhara kwao.

Alipomaliza kuongea uongo wake mimi nikasema kuwa tulipofikia ni bora itangazwe kuwa tuna mfumo mmoja wa juhudi, kwani sioni maana na uwepo wa juhudi mbadala kama utaratibu ndio huu wa kuchagua watu na kuhama kisha kuchagua tena.

Baada ya kumwambia hivyo naye akaja juu akasema pengine ni lengo ni juhudi mbadala kupandikiza mamluki ndani ya juhudi mkuu. Ili wakiingia kwenye maeneo nyeti ya juhudi mkuu watibue. Hii ikawa kichekesho ndani ya kichekesho cha kupuuzwa.

Binafsi niliyapuuza maoni hayo maana naona huu ni upigaji tu kama upigaji mwingine. Sema huu unaendesha kisomi zaidi baada ya kugundua udhaifu wa rubani wa juhudi. Ukitumia mwavuli wa chama utapiga pesa mpaka uchoke bila kuguswa.

Ila nawaonya wanaokubali mchezo huu wa kuunga juhudi wakikengeuka mbele ya safari huku faranga nyingi zimetumika kwa ajili yao, watakiona cha moto kutoka kwa wamiliki wa juhudi ndani ya taifa hili. Wasithubutu.

Kuna watu najua hawaelewi au hawakubaliani na hili. Kwamba kazi ya kupata mwenye juhudi safari hii ni mgumu kuliko. Mwenye juhudi na muunga juhudi wote watapata taabu sana. Juhudi zitabaki kuwa juhudi kama juhudi za kuchagua mwenye juhudi halisi.

Kwanza samahani, nilianza moja kwa moja na maneno mengi bila salamu. Kwa wale ambao mambo ya kiafya hayako sawa na kukaa tenge poleni sana. Lakini vipi jamani mnaonaje mfumuko wa bei?

Ujanjaujanja watiwa kufuli

Maana toka 2005 vitu bei iko juu mpaka leo halafu cha kushangaza mishahara imeganda palepale kama sanamu la askari pale posta katikati ya Dar es Salaam. Au ndo maana mpango mzima ni kuunga juhudi?

Maana kuniongezea elfu mbili katika mshahara wangu naona unazingua tu. Ni kuchezeana akili. Unaongeza elfu mbili halafu kila kitu bei juu kama minara ya simu maana yake nini? Kama si kunisanifu tu.

Ni kweli pesa za ujanjaujanja zimebanwa. Lakini ubanaji uende sambamba na udhibiti wa mfumuko wa bei. Muigeni Mzee Mkapa ambaye katika utawala wake alibana kila kitu mpaka neno la Ukapa likazaliwa, lakini alidhibiti mfumuko wa bei.

Awamu hii siyo Ukapa tena, bali milango ya pesa za ujanjaujanja wizi na ufisadi imetiwa kufuli. Lakini wamesahau kuweka kufuli katika mlango wa mfumuko wa bei. Hapa kubana ni sawa na kujaza maji kwenye pakacha.

Jamani huu wa wimbo wa amani msitegemee utaendelea kutufurahisha. Wakati tunawaona nyinyi pekee ndiyo mnafaidika zaidi na amani hii. Kuna kitu tunakiona baina yenu na sisi. Tofauti kubwa sana ya kimaisha.

Wakati nyinyi mkipata nafasi ya kuunga na kuungwa kijuhudi, sisi ndoto ya juhudi hatujui tutaota lini. Fanyeni hima mambo yakae sawa kabla ule msemo wa kama mbwai na iwe mbwai haujaingia katika vichwa vya wengi.

Watu wanataka unafuu wa maisha, hizo propaganda za juhudi na matamko yatosha.

Hii ni karne ya ishirini na moja, hakuna Mtanzania mjinga. Siku itafika ya mtu wa Masaki na Tandale wote kupita njia moja.

Chanzo: mwananchi.co.tz