Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Tanzania yakimbikiza maonesho ya vito Thailand

Vito Maonesho (600 X 333) Tanzania yakimbikiza maonesho ya vito Thailand

Thu, 7 Sep 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Ushiriki wa Tanzania katika Maonesho ya 68 ya Vito na Usonara katika jiji la Bangkok nchini Thailand umewavutia Wafanyabiashara mbalimbali wa madini kutokana na wengi kutumia malighafi za madini kutoka nchini.

Akizungumza baada ya kushiriki hafla fupi ya ufunguzi wa maonesho hayo, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo amesema wafanyabiashara wakubwa wa madini nchini humo wakiwemo viongozi wa Serikali wameonesha nia ya kushirikiana na Tanzania katika nyanja mbalimbali zikiwemo biashara ya madini, uongezaji thamani madini pamoja na kubadilishana uzoefu katika shughuli hizo.

Aidha, Mbibo amesema uwepo wa Tanzania katika maonesho hayo ya madini yenye thamani kubwa unalenga kujifunza pamoja na kuhamasisha urejeshwaji wa minada ya madini nchini na kuhamasisha uwepo wa masoko ya madini ambapo wafanyabiashara hao wanaweza kununua madini kupitia masoko ya madini yaliyoanzishwa katika kila mkoa nchini.

Serikali kupitia Wizara ya Madini inatarajia kurejesha tena minada ya madini nchini pamoja na Maonesho ya Kimataifa ya Vito na Usonara ya Arusha yatakayofanyika kila mwaka kulingana na kalenda za kimataifa ya maonesho ya madini ya vito na biashara za usonara.

Aidha, hivi karibuni Serikali kupitia Tume ya Madini ilitoa taarifa kuwa, Wizara ipo kwenye mchakato wa kuwasilisha mapendekezo ya maboresho ya Sheria na Kanuni ili kuwezesha maonesho na minada ya vito kufanyika nchini ikiwemo marekebisho ya Kanuni za Eneo Tengefu la Mirerani za Mwaka 2021 ambazo zilizuia kuuzwa kwa madini ya Tanzanite nje ya Mirerani.

Kufuatia hayo, Mbibo ametoa wito kwa wauzaji, wachimbaji, waongezaji thamani madini kutumia uhusiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na Thailand ambao umekuwepo kwa muda mrefu kuchangamkia fursa hiyo ikiwemo kuungana na wadau wa nchi hiyo katika masuala yanayohusu mnyororo wa shughuli za madini.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live