MHANDISI Mtafiti kutoka Kampuni tanzu ya Shirika la Umeme nchini, 'TGDC' Edgar Akilimali amesema punde itakapokamilika miradi ya TANESCO na kampuni zake tanzu, changamoto ya umeme nchini itakuwa historia kwani utazalishwa umeme wa kutosha kufikia kuuzwa katika nchi zenye uhitaji.
Akitaja vyanzo hivyo, Akilimali amesema mbali na chanzo kilichozoeleka cha umeme unaozalishwa kupitia maji ya mito na mabwawa, pia wameweka nguvu kwenye uzalishaji wa umeme kupitia nishati ya jua, upepo, gesi asilia, geo thermal, umeme wa maporomoko na vyanzo vingine.
Itakumbukwa kuwa hivi sasa Serikali inatekeleza miradi mikubwa ya kuzalisha umeme ukiwemo mradi wa Bwawa la Nyerere ambalo litazalisha megawati 2,115, pamoja na kujenga njia ya umeme ya 400kV yenye urefu wa kilometa 1,300 itakayounganisha nchi za mashariki na kusini mwa Afrika, ambapo tayari kilometa 900 za njia hiyo zimejengwa na umekamilika.