Tanznaia imejumuishwa kwenye orodha ya nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS) zitakazonufaika na utekelezwaji wa Programu ya Fit for Market Plus inayolenga kuwajengea uwezo wajasiriamali.
Programu hiyo pia inalenga kuwajengea uwezo wanaojihusisha na mnyororo mzima wa uongezaji thamani katika mazao ya kilimo, hususani mbogamboga na matunda ili waweze kuzalisha mazao na bidhaa za kilimo zinazokidhi viwango na mahitaji ya soko, hasa la Umoja wa Ulaya.
Taarifa ya Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki jana ilieleza kuwa programu hiyo inayotekelezwa na taasisi ya COLEACP kwa ufadhili wa Umoja wa Ulaya (EU) inazingatia mkakati unaolenga kudhibiti ubora wa bidhaa za mazao ya kilimo zinazoingia kwenye soko kuanzia shambani mpaka zinapomfikia mlaji wa mwisho.
“Kupatikana kwa fursa hiyo ni jitihada za Ubalozi wa Tanzania nchini Ubelgiji katika mikakati ya utekelezaji wa diplomasia ya uchumi ambao unawahimiza pia wadau kutembelea tovuti: www.be.tzembassy.go.tz ili kupata taarifa zaidi kuhusu fursa mbalimbali zinazopatikana kwenye eneo la uwakilishi la ubalozi huo,” ilieleza taarifa.