Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Tanzania kujitosheleza kwa sukari ifikapo 2024

1a9411770c0c7b5f7cac545b1074619c Tanzania kujitosheleza kwa sukari ifikapo 2024

Thu, 28 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

WAZIRI wa Kilimo, Profesa Adolf Mkenda amesema ifikapo mwaka 2024/2025 Tanzania itajitosheleza kwa sukari kutokana uzalishaji viwandani kuongezeka hadi kufikia tani 704,000, hivyo kuvuka mahitaji ya nchi wakati huo ya tani 568,371 na akiba itakuwa tani 135,629.

Akizungumza jijini hapa jana, Profesa Mkenda alisema pamoja na mahitaji ya sukari wakati huo 2024/2025 kuongezeka kutokana na ongezeko la vipato na idadi ya watu, mkakati uliopo wa serikali ni kuongeza uzalishaji wa sukari na kuachana na uagizaji nje ya nchi.

“Serikali inaendelea kufuatilia mpango wa upanuzi wa viwanda vya Kilombero, Kagera na Mtibwa vinavyotajarajiwa kuzalisha tani 519,000 ifikapo mwaka 2024/25,” alisema Waziri wa Kilimo.

Ukamilikaji wa viwanda hivyo na mchango wa uzalishaji kutoka kwenye miradi mipya ya Bagamoyo tani 35,000 na

Mkulazi tani 50,000 na hivyo uzalishaji unatarajiwa kufikia tani 704,000.

Kuhusu miwa ya wakulima kubaki shambani kwa uwiano wa hekta 10 tani moja ya sukari, Profesa Mkenda alisema iwapo eneo lote lingevunwa lenye miwa la hekta 57,640 sawa na hekta 37,624 za viwanda na za wakulima wadogo hekta 20,016, jumla ya tani 4,010,720 za miwa zingepatikana na zingezalisha tani 401,072 za sukari kwa mwaka .

Hata hivyo, kutokana na uwezo mdogo wa uchakataji miwa kwa viwanda vya Kilombero na Manyara kiasi cha miwa ya wakulima wadogo kinabaki shambani bila kuvunwa ambavyo ni jumla ya wastani wa tani 201,800 sawa na tani 195,550 kwa Kilombero na tani 6,500 kwa Manyara ambazo zingezalisha tani 20,000 za sukari.

Alikiiagiza Kiwanda cha Kilombero na vingine nchini, kuongeza na kuimarisha uwezo wa uchakataji miwa ili kunusuru hasara kubwa wanayoipata wakulima kutokana na kutovunwa miwa yao ambayo kama ingevunwa ingekuwa na thamani ya Sh bilioni 19.

“Serikali haitosita kuchukua hatua ya kuruhusu mwekezaji mwingine kujenga kiwanda cha kati au viwanda vidogo endapo mwekezaji aliyepo sasa katika Bonde la Kilombero atashindwa kufanya upanuzi unaostahili kwa wakati ili miwa ya wakulima wadogo takribani tani 200,000 inayobaki katika bode hilo ipate soko la uhakika,” alisema.

Profesa Mkenda alisema Bodi ya Sukari Tanzania na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) zinaendelea kutangaza maeneo yaliyoanishwa kwa ajili ya kilimo cha miwa na uzalishaji wa sukari ili kupata wawekezaji wenye nia ya kuwekeza kwenye sukari.

Alitaja maeneo hayo muhimu ambayo yanaweza kuzalisha wastani wa tani 976,000 za sukari kwa mwaka ni pamoja na Kibondo hekta 25,000 kuzalisha sukari tani 160,000, Kasulu hekta 37,000 kuzalisha tani 240,000, Rufiji hekta 25,000 kuzalisha tani 160,000 na Songwe hekta 22,000 kuzalisha tani 128,000.

Pia Mara hekta 12,000 kuzalisha tani 48,000 za sukari, Mpanda hekta 27,462 kuzalisha tani 160,000 na Rukwa hekta 12,372 kuzalisha tani 80.

Profesa Mkenda alisema uzalishaji wa sukari kwa mwaka ni wastani wa tani 300,000 ambapo katika msimu wa mwaka 2020/21 jumla ya tani 377,527 zitazalishwa kutoka viwanda vya Kilombero, Mtibwa, Kagera, TPC Moshi na Manyara.

“Kwa ujumla mahitaji ya sukari nchini kwa matumizi ya kawaida na viwandani ni tani 655,000 kwa mwaka, kati ya hizo tani 490,000 zikiwa na ziada ya tani 70,000 sawa na mahitaji ya miezi mwili ni sukari ya matumizi ya kawaida na tani 165,000 ni matumizi ya viwandani.

“Kutokana na uzalishaji huo, sukari inayozaishwa nchini haitoshelezi mahitaji ya soko la ndani na hivyo nchi huagiza wastani wa tani 40,000 za sukari ya matumizi ya kawaida kufidia pengo la mahitaji halisi ya sukari nchini kwa matumizi ya kawaida,” alisema waziri huyo.

Mwenyekiti wa Bodi ya Sukari, Mwamini Malemi alisema lengo la bodi hiyo ni kuhakikisha serikali inapunguza uagizaji wa sukari kutoka nje ya nchi kwa kuongeza uzalishaji viwandani ambavyo vinatakiwa kuchakata miwa yote kutoka kwa wakulima ili wananchi wapunguze umasikini.

Chanzo: habarileo.co.tz