Mwanza. Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) linajipanga kununua kivuko, magari na boti kwa ajili ya kukuza sekta ya utalii nchini.
Hayo yameelezwa leo Alhamisi Julai 4, 2019 na kamishna msaidizi wa shirika hilo, Paul Banga na kubainisha kuwa kivuko hicho kitakuwa na uwezo wa kupakia abiria 100
Alitoa kauli hiyo wakati akitoa mada kuhusu uanzishwaji hifadhi mpya na fursa za uwekezaji zilizopo nchini Tanzania katika mkutano wa mwaka wa Tanapa unaofanyika jijini Mwanza na kuhudhuriwa na wahariri na waandishi waandamizi kutoka vyombo mbalimbali vya habari.
Amesema kivuko na boti zitasaidia kusafirisha watalii katika hifadhi ya Lubondo, Burigi-Chato, kisiwa cha Saanane, Rubondo, Rumanyika-Korogwe na Ibanda -Kyerwa.
Banga amesema katika hifadhi hizo mpya wametenga maeneo ya uwekezaji ya ujenzi wa hoteli.