Serikali kupitia Tume ya Mipango imesema kuwa itafanya tafiti kwa lengo la kubaini fursa za maendeleo katika maeneo mbalimbali nchini.
Hayo yamebainishwa leo Februari 2 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo wakati akijibu maswali ya Wabunge ambapo alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Neema Mwandabila aliyetaka kujua Serikali ina mkakati gani wa kufanya utafiti maalumu katika Mji wa Tunduma ili kubaini ni namna gani unaweza kuchangia kukuza uchumi wa nchi.
“Kwa mujibu wa Sheria ya Tume ya Mipango, hususani Kifungu cha 6(2), pamoja na majukumu mengine, Tume ya Mipango ina jukumu la kufanya utafiti kuhusu suala lolote ambalo Tume inaona ni muhimu katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa.
Kwa kuzingatia hili, Tume ya Mipango imejipanga kufanya tafiti mbalimbali na kuratibu tafiti zitakazofanywa na taasisi nyingine (za umma na binafsi) kwa lengo la kubaini fursa za maendeleo katika maeneo mbalimbali nchini.” Amesema Prof. Mkumbo.