Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Taboa yasitisha mgomo wa mabasi

Ba4e24270d7f34083013ff69c82b298f Taboa yasitisha mgomo wa mabasi

Sat, 13 Mar 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

CHAMA cha wamiliki wa Mabasi Tanzania (TABOA) kimesitisha mgomo wa mabasi iliokuwa imeuitisha hapo awali kwa ajili ya kusubiri majibu ya kamati shirikishi ya pamoja inayoundwa na wajumbe kutoka LATRA, TRA pamoja na NIDC kwa ajili ya kutafuta majibu ya changamoto iliyowafanya kuitisha mgomo huo.

Awali mwishoni mwa wiki iliyopita Taboa kupitia kwa kamati yake ya utendaji ilikutana na wanachama wake na kwa pamoja waliazimia kusitisha kutoa huduma za usafiri wa mabasi yao kwa kile walichodai wanapata hasara kutokana na kutumia mfumo wa ukatishaji wa tiketi mtandao.

Kwa mujibu wa Naibu Katibu Mkuu wa Taboa, Priscus John, changamoto mbalimbali zinazotokanazo na mfumo huo, zimekuwa nyingi kiasi cha kuwafanya kupata hasara ambayo mbali na kukatwa asilimia mbili ya fedha wanazoweka kwa ajili ya kutoa huduma na Latra, pia mfumo huo unachelewesha kufanyika kwa malipo hivyo kuwaweka katika wakati mgumu pale wanapotaka kuongeza salio ndani ya mfumo kwa ajili ya kuendelea kukatisha tiketi wa abiria.

“Tumekuwa katika kikao cha pamoja na viongozi wa Latra, TRA na NIDC kwa ajili ya kujadiliana kwa kina kuhusu changamoto hiyo, kimsingi hadi sasa jambo hili halipo vibaya sana kwa kuwa tumekubaliana kuunda kamati ya kufuatilia kwa kina suala hili na baadae itakuwa na majibu wamefikia wapi,” alisema John.

Alisema wameyapokea maamuzi hayo kwa mikono miwili kwa kuwa imani yao kupitia kamati hiyo changamoto inayowakabili itaweza kupatiwa ufumbuzi ikizingatiwa kuwa kutoa huduma kwa wananchi ndiyo jukumu kubwa walilonalo.

“Tupo hapa kumuunga mkono Rais wetu John Magufuli kutoa huduma kwa wananchi, hatuna mpango wa kugoma, isipokuwa changamoto tunazokutana nazo wakati wa utoaji wa huduma hizo ndizo zinatupelekea kufikiria kusimamisha mabasi kutoa huduma kwa kuwa zinatubana,” aliongeza Naibu Katibu Mkuu huyo.

Kimsingi alisema wao kama wasafirishaji wanaona vyema kuendelea kutumia utaratibu wa ukatishaji tiketi kupitia mfumo wa EFD kwa kuwa haukuwa na changamoto nyingi kama ambavyo mfumo huo wa tiketi mtandao ulivyo sasa.

Gazeti hili lilipowatafuta viongozi wa Latra ili kuzungumzia kwa kina suala hilo hawakuweza kupatikana baada ya simu zao kutopokelewa, juhudi za kuwatafuta zinaendelea

Chanzo: www.habarileo.co.tz