Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

TRC yajivunia kujenga reli ya kisasa ndefu Afrika

SGR 1 TRC yajivunia kujenga reli ya kisasa ndefu Afrika

Mon, 3 Apr 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

MKURUGENZI Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa amesema Tanzania ni nchi ya kwanza Afrika inayojenga reli ya kisasa yenye urefu wa kilometa 2,102.

Akizungumza hivi karibuni jijini Dodoma, Kadogosa alisema: “Ujenzi wa reli ya kisasa urefu wa kilometa 2,102 unaifanya Tanzania kuwa nchi itakayokuwa na reli ya kisasa ndefu zaidi Afrika”.

Kwa ujenzi wa reli hiyo ya kisasa Dar es Salaam hadi Mwanza pamoja na kipande cha Tabora hadi Kigoma, serikali itakuwa imewekeza jumla ya Dola za Marekani bilioni 10.04 sawa na Sh trilioni 23.3.

Huo ni uwekezaji mkubwa uliofanywa na serikali katika ujenzi wa reli hiyo ya kisasa katika awamu ya kwanza Dar es Salaam – Mwanza pamoja na kipande cha Tabora – Kigoma.

Kadogosa alisema ujenzi wa vipande vya Dar es Salaam hadi Morogoro, Morogoro – Makutupora na vipande vya Mwanza – Isaka, Makutupora – Tabora, Tabora – Isaka vyote vina wakandarasi na wanaendelea na kazi za ujenzi.

Ujenzi wa kipande cha Tabora – Kigoma upo katika hatua za mwisho za kukamilisha manunuzi.

Ujenzi wa reli ya kisasa kati ya Tabora – Kigoma una jumla ya kilometa 506 ambapo njia kuu ni kilometa 411 na njia za kupishania kilometa 95.

Ujenzi huo utakuwa na stesheni 10 kutoka Tabora mpaka Kigoma na vituo vikubwa viwili vya mizigo.

Thamani ya mkataba wa ujenzi huo ni Sh trilioni 6.34 ambapo ujenzi huo unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi 48 sawa na miaka miwili.

Ujenzi wa kipande cha Tabora- Kigoma utaifanya reli nzima tangu Dar es Salaam-Mwanza na Tabora-Kigoma kuwa na jumla ya urefu wa kilometa 2,102 ambapo njia kuu ni kilometa 1,633 na njia za kupishania kilometa 469.

Ujenzi wa awamu ya kwanza ya kipande cha kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro umefikia zaidi ya asilimia 97.67, kipande cha Morogoro – Makutupora umefikia zaidi ya asilimia 91.32, kipande cha Makutupora – Tabora ni asilimia 3.26, kipande cha Tabora – Isaka ni zaidi ya asilimia 0.49, na kipande cha Isaka – Mwanza ni zaidi ya 19.70.

Alisema manunuzi ya ujenzi wa tawi la Uvinza hadi Itega, Burundi unaendelea, reli hiyo pia itaunganisha bandari ya Dar es Salaam na DRC kupitia bandari ya Kigoma. Katika ujenzi huu reli hiyo itaifikia miji mitatu yenye watu wengi ndani ya DRC ambayo ni fursa kwa wafawafanyabiashara.

“Kwa ujumla ujenzi wa awamu ya kwanza ya kipande cha kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro umefikia zaidi ya asilimia 97.67, kipande cha Morogoro – Makutupora umefikia zaidi ya asilimia 91.32, kipande cha Makutupora – Tabora ni asilimia 3.26, kipande cha Tabora – Isaka ni zaidi ya asilimia 0.49, na kipande cha Isaka – Mwanza ni zaidi ya 19.70,” alisema.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live