Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

TRA: Wafanyabiashara lipeni kodi kwa wakati

TRAA TRA: Wafanyabiashara lipeni kodi kwa wakati

Thu, 18 Jun 2020 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imewataka wafanyabiashara ambao hawajakadiriwa Kodi ya mapato kwa kipindi kinachoishia Marchi 31, mwaka huu kufika katika ofisi za mamlaka hiyo kukadiriwa na kulipa Kodi zao kabla ya Juni 30,2020.

Hayo yamezungumzwa leo jijini Mbeya na Kaimu Meneja wa Elimu kwa Mlipakodi wa TRA, Stephen Kauzeni ambaye amewahimiza hayo wakati wa kampeni ya uhamasishaji wa ulipaji kodi inayoendelea mkoani humo.

Aidha amewakumbusha wafanyabiashara wote ambao mwaka wao wa mahesabu unaishia Desemba 31,2019 kuwasilisha ritani zao TRA kabla ya mwisho wa mwezi huu.

Amesema kwa upande wa wafanyabiashara wanaolipa kwa awamu lakini bado hawajakadiriwa kodi zao ni vyema wakafika TRA ili wakadiriwe na walipe mapema kabla ya tarehe ya mwisho ili kuepuka adhabu na riba.

“Tunawatembelea wafanyabiashara kwenye maeneo yao ya biashara ili kuwakumbusha na kuwahimiza wale ambao bado hawajafanyiwa makadirio, wakakadiriwe na wawahi kulipa kodi zao kwa wakati bila bughudha kuliko kusubiri siku ya mwisho kabisa”, amesema.

Kauzeni ameongeza kuwa, kutokana na janga la ugonjwa wa korona, TRA isingependa kuona msongamano wa watu katika ofisi zake na kwamba imewalazimu maofisa wake kuwafuata walipakodi kwenye maeneo ya biashara zao ili kuwapa elimu ya kodi na kuwasisitiza wakailipe kwa.

“Ni wajibu wa mlipakodi kulipa kodi zake kwa wakati lakini pia TRA ina wajibu wa kutoa elimu pamoja na kumkumbusha mlipakodi kulipa kodi na ndiyo maana tumewafuata huku madukani kwao kuwapatia elimu na kuwahimiza kulipa kodi kwa wakati,’’ amesema Kauzeni.

Amesema kwa wafanyabiashara ambao mwaka wao wa hesabu unaishia Desemba 31, 2019 wanatakiwa kuhakikisha wanawasilisha ritani zao kabla au Juni 30, 2020 ili ritani zao ziweze kuhakikiwa na kufanyiwa kazi kwa wakati kwa mujibu wa sheria za kodi zinavyoelekeza.

“Niwasihi walipakodi wafuate sheria ya Usimamizi wa kodi na kuwasilisha ritani zao ziweze kufanyiwa kazi mapema”, amesisitiza Kauzeni.

Kauzeni amesema kampeni hii ya uhamasishaji ulipaji kodi kabla ya Juni 30, 2020 inalenga kuwakumbusha walipakodi kulipa kodi zao kwa wakati pamoja na kuongeza hamasa ya ulipaji kodi kwa hiyari miongoni mwa wafanyabiashara na watoa huduma zinazolipiwa kodi kama vile mawakili, wahasibu na fani zingine zilizosajliwa.

Amesema kampeni hii ya utoaji elimu na uhamasishaji ulipaji kodi kwa wakati na hiyari inaendelea katika mkoa wa Mbeya na wilaya zake.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live