Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

TBS yataja sababu, faida ukaguzi magari Dar

8579acc4be97474f54ce722f9cbf6601 TBS yataja sababu, faida ukaguzi magari Dar

Fri, 22 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limesema kupima viwango vya ubora kwa magari nchini kutasaidia kuongeza ajira na kuokoa fedha za kigeni zilizokuwa zikilipwa kwa mawakala wa nchi za nje.

Shirika hilo limesema lina jozi 12 za vifaa vya teknolojia ya kisasa kupima ubora huo.

TBS ilisema jana kuwa, wakati magari yanapimwa nje mwenye gari alilipa Dola za Marekani 150 na kwamba shirika hilo lilipata asilimia 30 ya fedha hizo lakini sasa gharama itakuwa dola za Marekani 140 na tozo ya huduma Sh 30,000.

Kwa kuzingatia viwango hivyo mwenye gari sasa atalipa kati ya 300,000 hadi 350,000 za ukaguzi wa gari katika Bandari ya Dar es Salaam.

Akizungumzia uamuzi wa TBS kusitisha ukaguzi wa ubora kwa magari nje ya nchi, Mkurugenzi wa Udhibiti wa Ubora katika shirika hilo, Lazaro Msasalaga, alisema uamuzi huo umefanywa ili kuleta ajira kwa Watanzania, kuokoa fedha na pia nchi kuwa na uzoefu.

Alisema hivi sasa TBS ina uwezo wa kufanya ukaguzi na utafanyika kwa magari yanayotumika nchini na si yanayopita kwenda nchi nyingine.

Msasalaga alisema ukaguzi utafanyika baada ya kukamilika kwa taratibu zote za kutoa gari bandarini.

Msasalaga alisema ukaguzi huo utafanywa kwa kutumia vifaa vya teknolojia ya kisasa ambavyo wamevigawa katika yadi nne ili kurahisisha ukaguzi.

Alisema yadi ya kwanza itakuwa na jozi nane za vifaa vya kupima viwango vya magari madogo na yadi ya pili) itakuwa na jozi mbili za kupima magari makubwa.

Msasalaga alisema, yadi ya tatu ijulikanayo kama yadi ya Kitopeni itakuwa na jozi moja ya vifaa hivyo kwa ajili ya kupima magari ya aina mbalimbali na jozi moja itafungwa eneo la UDA kwa ajili ya kupima magari yaliyopimwa na kukutwa hayana viwango na kupelekwa kutengenezwa kisha kukaguliwa upya.

Alisema gari ambalo halitaweza kukidhi vigezo halitasajiliwa na kwa mujibu wa sheria ya udhibiti viwango inatakiwa kuharibiwa au kurudishwa lilipotoka lakini akabainisha kuwa wanaamini kwa elimu watakayotoa kwa waagizaji magari kasoro zitakuwa ndogo ndogo.

Alisema kila nchi inayouza magari yaliyotumika ina utaratibu wa kuyakagua kila mwaka au baada ya miaka miwili hivyo ni vema kwa waagizaji kuhakikisha wanaagiza magari yenye nembo za nchi husika kuwa yamekaguliwa na yana ubora.

“Ukaguzi huu utafanyika ndani ya bandari baada ya mawakala kukamilisha taratibu zote na tutahakikisja upimaji huo hauathiri uondoshaji wa magari bandarini ...gari halitasajiliwa mpaka tuhakikishe linakidhi viwango na gharama zote za upimaji zitakuwa za muagizaji magari,”alisema Mkurugenzi huyo.

Msasalaga alisema magari yanayoingia nchini kutoka nje ya nchi ni 30,000 hadi 40,000 kwa mwaka hivyo kila saa moja watapima magari 48 kutokana na mahesabu waliyofanya ambayo wana uhakika haitasababisha mlundikano wa magari bandarini.

Alitaja wadau wanaohusika na programu hiyo kuwa ni waagizaji wa magari, mawakala bandarini, taasisi za serikali ikiwemo bandari, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na taasisi za udhibiti ambazo kwa pamoja watakutana kuangalia namna ya kufanikisha programu hiyo.

Alisema mwaka 2002,TBS ilianza kupima viwango vya magari kwa kutumia mawakala baada ya mchakato wa zabuni kwa kufuata sheria ya manunuzi kwa mkataba wa miaka mitatu na kutoa vyeti kwa niaba ya TBS.

Alisema programu hiyo ilikuwa na mafanikio kwani ilisaidia kuingia nchini magari yaliyokidhi viwango na kwa kuwa si lazima kukagua magari nje ya nchi kila nchi inauwezo wa kukagua kulingana na matakwa yake.

Chanzo: habarileo.co.tz