Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

TBS yasisitiza viwango bidhaa madukani

Fd7266ac0ca5eee571369abd53f6a300.png TBS yasisitiza viwango bidhaa madukani

Wed, 21 Apr 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limewataka waingizaji na wauzaji wa bidhaa kuhakikisha wanaingiza bidhaa ambazo ni bora na salama ili kukuza biashara na kuepuka kupoteza masoko .

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Mkuu wa Kanda ya Magharibi (TBS), Rodney Alananga wakati wa ukaguzi wa kushtukiza sokoni kwa wasambazaji na wauzaji wa bidhaa mbalimbali vikiwemo vilainishi, vipuri vya magari, vifaa ya ujenzi, chakula na vipodozi .

Alisema wasipofuata maelekezo hayo na shirika hilo likawabaini itawalazimu kuziteketeza bidhaa hizo kwa gharama zao.

Alisema katika ukaguzi uliofanyika Kanda ya Magharibi Mkoani Kigoma katika wilaya za Kakonko, Kibondo, Buhigwe, Kasulu, Uvinza na Kigoma shirika lililenga kuhakiki iwapo bidhaa zinazouzwa sokoni kama zimekidhi ubora wa kiwango husika.

Pia alisema ukaguzi huo ulienda sambamba na utoaji elimu kwa wauzaji na wanunuaji juu ya uhifadhi sahihi wa bidhaa na umuhimu wa kuzingatia na kusoma taarifa sahihi na muhimu katika vifungashio.

TBS imefanya ukaguzi huu sambamba na usajili wa majengo ya chakula na vipodozi ili kuhakikisha majengo yanazingatia ubora na usalama wa bidhaa za chakula na vipodozi vinavyohifadhiwa au vinavyouzwa.

Kwa upande wake Ofisa Usalama wa Chakula (TBS ), Elisha Meshack alisema ukaguzi huo ni endelevu kwani ni moja ya majukumu ya shirika na utahusisha bidhaa mbalimbali katika sekta zote kasoro dawa .

"Huu ni mwendelezo tu wa shughuli zetu za kila siku, kwani shirika linahakikisha ukaguzi kama huu unafanyika katika kila wilaya nchi nzima ili kuhakikisha tatizo la bidhaa hafifu linapungua kwa kiasi kikubwa kama sio kwisha kabisa,"alisema.

Ofisa Udhibiti Ubora(TBS), Emmanuel Mushi aliwasisitiza wafanyabiashara wa maduka ya chakula na vipodozi ambao wamefanyiwa ukaguzi na kupewa gharama za malipo na bado hawajalipia gharama za usajili kulipia mara moja ili wapate kibali cha kuuza bidhaa husika katika majengo hayo ili kuepuka usumbufu na wale ambao hawajasajili majengo yao kusajili mara moja.

Meneja wa kiwanda cha kuzalisha maji wilayani Kibondo cha Malagarasi Mineral General Supply", Samir Adam ameipongeza TBS kwa kusogeza huduma karibu na amekuwa akipata ushirikiano wa kutosha kutoka ofisi ya kanda ya magharibi, Kigoma.

Pamoja na ukaguzi huo TBS, inatumia fursa hiyo ya kukutana na mfanyabiashara mmoja mmoja kuelezea majukumu ya shirika ikiwa ni pamoja na yale yaliyokuwa yakifanywa na iliyokuwa Mamlaka ya Chakula na Dawa ( TFDA).

Chanzo: www.habarileo.co.tz