Shirika la viwango Tanzania (TBS) wamewataka wananchi kufuata maelekezo yanayotolewa kwenye vinywaji, ili kuepuka madhara ya kiafya.
Kumekuwa na malalamiko kutoka kwa watumiaji wa vinywaji ikiwamo pombe kali na vile vya kuongeza nguvu 'energy drinks' kuwa vina madhara kwa watumiaji.
Hayo yamesemwa leo Aprili 15,2023 jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Udhibiti Ubora wa TBS, Lazaro Msasalaga katika mkutano wa wahariri na waandishi wa habari.
"Wapo watu wanakunywa zaidi ya kiwango kilichowekwa na wengine bila kula. Hapo wanavitumia tofauti na maelekezo yaliyowekwa na watengenezaji," amesema Msasalaga.
Amesema vinywaji vyote vilivyopo katika soko vimepitiwa na TBS, hivyo vipo salama kwenye matumizi muhimu ni kuzingatiwa matumizi sahihi kwa kufuata maelekezo.