Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

TBL yawezesha wakulima 100 kushiriki maonesho ya TARI

9203f5867a0b15e97c1eaa6b185ec0c7 TBL yawezesha wakulima 100 kushiriki maonesho ya TARI

Thu, 30 Jul 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

Katika mkakati wake wa kuwainua wakulima nchini Kampuni ya Tanzania Breweries (TBL), imewezesha wakulima wa zao la shayiri Kanda ya Kaskazini inaoshirikiana nao, kushiriki maonesho ya kilimo yaliyofanyika Arusha yaliyoandaliwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo nchini (TARI).

Meneja Kilimo wa TBL, Joel Msechu alisema kampuni imedhamini wakulima wapatao 100 kuhudhuria maonesho hayo kwa ajili ya kujifunza mbinu za kilimo cha kisasa na matumizi ya teknolojia katika kuleta mapinduzi ya kilimo ili ziwasaidie kuongeza uzalishaji. Alieleza kuwa kwa kipindi kirefu, kampuni hiyo imekuwa ikishirikiana na wakulima wa zao hilo kwa kuwapatia mbegu bora, zinazofaa katika hali ya hewa ya maeneo yao na kuwahakikishia soko la uhakika wa mavuno yao. Hatua hiyo imewezesha wakulima hao kuongeza uzalishaji.

“Kwetu TBL tunaamini ushirikiano unaweza kuchochea kuleta maendeleo endelevu. Maonesho ya kilimo ni moja ya fursa ya kuwakutanisha wakulima wetu wa mazao ya shayiri na mtama na kuwawezesha kupata maarifa ya kukabiliana na changamoto wanazokutana nazo katika kazi yao”,alisema Msechu.

Kampuni ya TBL imedhamiria kuunga mkono jitihada za Serikali ya Tanzania, za kuleta mapinduzi ya viwanda kupitia kuwekeza katika sekta ya kilimo ambapo inashirikiana na wakulima 6,000 wa zao la shayiri katika mikoa ya Kilimanjaro, Manyara, Arusha na Iringa. Pia, kampuni inajenga kiwanda cha kusindika kimea mkoani Dodoma, ambacho kitakuwa na uwezo wa kuzalisha tani 32,000 za kimea.

Kwa sasa kampuni inanunua asilimia 74 ya malighafi zake nchini na imedhamiria kuongeza zaidi matumizi ya malighafi kutoka nchini katika miaka ijayo.

Chanzo: habarileo.co.tz