Arusha. Benki ya Maendeleo ya Kilimo nchini(TADB) imewahakikishia wakulima kuwa inao mtaji wa kutosha na kuwataka kuitumia benki hiyo kuchukua mikopo ili waweze kuongeza tija katika kazi zao.
Hayo yalibainishwa na meneja wa biashara wa TADB, Dickson Pangamawe jana jioni Desemba 8, wakati wa ufunguzi wa maonyesho ya taasisi za fedha zinazojishughulisha na utoaji mikopo kwa wakulima yaliyoandaliwa na chama cha wakulima wa maua na mbogamboga Tanzania (Taha)
Pangamawe amesema benki hiyo inawahudumia wakulima wadogo waliojiunga kwenye vikundi, wakulima wa kati na wakubwa kwa kushirikiana na Taha ambayo inatoa utaalamu kwa wakulima.
"Serikali inalenga kuwasaidia wakulima kufikia malengo yao nitoe wito kwa wakulima kote nchini waitumie kuchukua mikopo ili walime kibiashara kufikia malengo ya serikali ya kuwa na uchumi wa viwanda," amesema Pangamawe
Mwenyekiti wa Bodi ya Taha, Erick Ng'imaryo amesema lengo la kuzikutanisha taasisi za fedha na wakulima ni kutengeneza jukwaa rafiki la kuzikutanisha pande mbili kujadiliana namna wakulima wanavyoweza kupata mikopo nafuu.
Alisema mwitikio wa wakulima umekua mzuri kwani wamepata nafasi ya kufahamu namna ya kupata mikopo ya kilimo, miundombinu ya umwagiliaji na kuunganishwa na masoko ya bidhaa zao hapa nchini na nje ya nchi.