Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Stempu ya WTTC kwa Tanzania iongeze kasi ya watalii nchini

WTTC Stempu ya WTTC kwa Tanzania iongeze kasi ya watalii nchini

Thu, 13 Aug 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

TAARIFA za Baraza la Dunia la Usafi ri na Utalii (WTTC) kwamba Tanzania ni miongoni mwa nchi salama zaidi duniani kutembelewa, zinarejesha matumaini ya sekta hiyo kustawi na kurejea kuwa moja ya sekta muhimu kwa uchumi wa taifa. Ilichangia asilimia 17.6 katika Pato la Taifa mwaka 2019.

Sekta ya utalii nchini kama zilivyo nchi nyingine, kuanzia mapema mwaka huu, ilipata athari kubwa baada ya mipaka na anga za nchi nyingi duniani kufungwa ili kudhibiti mlipuko wa ugonjwa wa homa kali ya mapafu, unaosababishwa na virusi vya corona (Covid-19).

Jitihada zilizofanywa na Tanzania kuukabili ugonjwa huo na matokeo chanya ya namna mipango madhubuti ya kuhakikisha usalama kwa wageni wanaoingia nchini kabla, wakati na baada ya corona ni moja ya sababu za WTTC kuitaja kuwa miongoni mwa nchi salama zaidi duniani kutembelewa.

Hatua hii inaliweka taifa katika nafasi kubwa kupokea mamilioni ya watalii, ambao hata kabla ya Baraza hilo kuitaja, walishaanza kumiminika nchini kutokana na kupata uhakika wa usalama na namna serikali ilivyojipanga kuwapokea na kuwafuatilia kwa karibu na kuwapa huduma za kiwango cha juu wakati wote wawapo hapa nchini.

Lakini ajira katika sekta hii, zitaimarika hasa kutokana na takwimu za hivi karibuni za WTTC, zilizobainisha kuwa ajira za watu milioni 50 katika sekta ya utalii ziko hatarini kupotea duniani ikiwa ni anguko la kati ya asilimia 12 na 14.

Kutajwa kwa Tanzania kuwa nchi salama duniani kutembelewa, kumefanyika sambamba na utoaji wa nembo (Stempu) ambayo matumizi yake yalielezwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamis Kigwangalla alipoizindua hivi karibuni.

Katika uzinduzi huo, Dk Kigwangalla alinukuliwa akisema stempu hiyo itawapa uhakika watalii kuja nchini na itasaidia kuongeza idadi yao kwa kuwa wengi wao kabla ya kufanya uamuzi wa kutembelea nchi yoyote, huwa wanataka kujihakikishia usalama wa nchi husika kuanzia ulinzi, huduma za vyakula, malazi na usafiri.

Kwa mujibu wa Kigwangalla, stempu hiyo tutaanza kuiona katika kila tangazo linalohusu utalii wa Tanzania. Hakika haya ndio matokeo chanya ya mageuzi makubwa ya kisekta yaliyofanywa na serikali kwa muda mrefu.

Nafahamu kuwa wadau wa sekta hii wakiwamo serikali kupitia wizara yenye dhamana, wenye hoteli, kampuni za utalii, usafiri wa anga na wa ardhini, wamekuwa na vikao na mikutano ya mara kwa mara kuweka mikakati mbalimbali ya kuboresha utalii nchini.

Nakumbuka mara zote ndoto za Rais John Magufuli ni kuifanya Tanzania nchi mdhamini barani Afrika. Hili litawezekana kwa kuendelea kuongeza nguvu ya pamoja kati ya serikali na sekta binafsi kuhakikisha maeneo yanayochochea kasi ya ukuaji wa uchumi kama utalii, yanawekewa nguvu ya ziada na uzalendo mbele ili kufikia malengo.

Kikubwa na cha muhimu ni kuhakikisha ushirikishwaji, ushirikiano na utendaji kazi wa pamoja, unaongezeka katika kuitangaza nchi na vivutio vyake kila kona kupitia vyombo vya habari vya ndani na nje, mitandao ya kijamii, mazungumzo ya ana kwa ana na njia nyingine salama ili kutumia vyema fursa hii.

Kama alivyosema Mkurugenzi wa Bodi ya Utalii Nchini (TTB), Devotha Mdachi kuwa idadi ya watalii nchini inaongezeka na kwamba wamejipanga kuhakikisha inalinda hadhi ya stempu hiyo ili itumike kuendelea kuwavutia watalii zaidi, binafsi naamini hii si kazi yao pekee yao bali Watanzania wote

Chanzo: habarileo.co.tz