Dar er Salaam. Shirika la Umeme (Tanesco) limetangaza kuwa kuanzia jana hadi Februari 13, baadhi ya maeneo ya mikoa ya Pwani, Dar es Salaam na Zanzibar yatakuwa yakikosa umeme mara kwa mara kutokana na ukarabati wa mashine za kufua umeme kwa gesi za Ubungo II.
Meneja uhusiano wa Tanesco, Leila Muhaji aliiambia Mwananchi jana kuwa kwa siku kukatika kwa umeme hakutachukua muda mrefu kama baadhi ya wateja wao wanavyodhani na wala hakuna mgawo.
“Mikoa hiyo haiwezi kuingia gizani. Watu wasiingiwe na hofu na hatuna mgawo,” alisema Leila.
Alisema ukarabati huo hufanyika kulingana na maelekezo ya matumizi ya mitambo hiyo.
“Hii mitambo inatakiwa itembee kwa saa 40,000 kulingana na maelekezo kisha inafanyiwa ukarabati, ni kama mtu anavyopeleka gari yake gereji ikiwa imetembea kilomita kadhaa.”