Katibu Mkuu wa Umoja wa Walimu wa Shule Binafsi nchini, Peter Mabula amesema sheria za kodi zinawakandamiza wawekezaji wadogo wa ndani kutokana na kuwepo utitiri wa kodi, tozo na michango ya lazima hali inayosababisha adha kubwa kwa wawekezaji hao huku akitolea mfano wa mwanamke aliyefiwa na mumewe kwa kubambikiwa kodi.
Mabula ametoa ushuhuda huo mbele ya Waziri wa Fedha Dk Mwigulu Nchemba, kwenye Jukwaa la Kodi na Uwekezaji Februari 28, 2024 jijini Dar es Salaam.
Jukwaa hilo lililobeba kaulimbiu isemayo Maboresho ya Sera katika Uwekezaji, Ukusanyaji wa Mapato ya Ndani na Ukuaji wa Uchumi Jumuishi lilifunguliwa na Makamu wa Rais Dk Philip Mpango kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.