SHAMBA la Kapunga Rise Project lililopo katika Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya, limetoa Sh. milioni 750 kujenga kituo cha afya kilichopo kwenye Kijiji cha Kapunga ili kuwasaidia wananchi kuepukana na tatizo la kutembea umbali wa kilomita 25 kufuata huduma za afya.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kupokea cheti cha shukrani kilichotolewa na Ofisi ya Wilaya ya Mkuu wa Wilaya Mbarali kwa kutambua mchango wao wa kujenga Kituo cha Afya cha Kapunga, Ofisa Habari na Mahusiano wa shamba hilo, James Malick, alisema waliamua kujenga kituo hicho kwa gharamza zao wenyewe ili kuendelea kudumisha uhusiano baina yao na wananchi wanaozunguka shamba hilo.
Alisema hadi sasa kituo hicho kimekamilika na kinaendelea kutoa huduma za matibabu baada ya kukamilisha ununuzi wa vifaa vyote vya matibabu.
“Kutokana na mahusiano mazuri tulionayo baina ya shamba letu wananchi wa kapunga, lakini na adha wanayopata kufuata huduma ya afya maeneo mengi ambapo hutumia kilomita 25, tuliamua kujenga kituo cha afya kwenye kijiji hicho ambacho kiko kwenye kata ya Itamboleo,” alisema Malick.
Akikabidhi cheti cha shukrani, Mkurugenzi wa Wilaya ya Mbarali, Kivuma Msangi, alipongeza hatua ya shamba hilo kuamua kujenga kituo cha afya, ili kuokoa maisha ya wananchi hususani wajawazito na watoto.
Aliwahamasisha wadau wengine kujitolea kwenye shughuli mbalimbali za maendeleo ikiwamo ujenzi wa vituo vya afya, shule na barabara ili kuwasaidia wananchi kupata huduma bora na kwa wakati.