Arusha. Serikali imepanga kuhakikisha vijiji vyote nchini, vinakuwa na mawasiliano ya simu ambapo vijiji 369 vinatarajiwa kujengwa minara ya mawasiliano.
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye ametoa taarifa hiyo leo Septemba 24, 2018 wakati akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufungua mkutano wa wadhibiti wa mawasiliano katika ukanda wa nchi za Afrika ya Mashariki.
Nditiye amesema mpango wa kujengwa minara hiyo, unatekelezwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) na unalenga kuhakikisha Watanzania wote wanawasiliana.
Mkuu wa uendeshaji wa UCSAF Mhandisi, Albert Richard amesema, katika awamu ya kwanza ya mpango huo, zabuni ilitangazwa kwa vijiji 218 kujengwa minara, ujenzi ambao ungegharimu Sh25.5 bilioni.
Hata hivyo, Mhandisi Richard amesema hadi sasa tayari zabuni imetolewa kwa vijiji 193 kujengwa minara kwa gharama ya Sh20.5 bilioni.