Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge leo amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa China nchini Wang Ke katika ofisi za wizara hiyo zilizopo Dodoma ambapo wamejadili masuala mbalimbali ikiwemo ufuatiliaji wa maendeleo ya miradi na programu mbalimbali zinazotekelezwa kwa ushirikiano kati yaTanzania na China.
Balozi Ibuge ameeleza kuwa uhusiano mzuri wa kidiplomasia baina ya Tanzania na China kumechagiza kwa kiasi kikubwa kukuwa kwa biashara, utali na uwekezaji baina ya nchi hizo mbili, hivyo urafiki wa mataifa hayo unapaswa kulindwa, kudumishwa na kuendelezwa katika hali yoyote.
“China kwa muda mrefu imekuwa ikichangia kwa kiasi kikubwa katika maendeleo ya Taifa letu kupitia sekta mbalimbali kama vile ujenzi wa mundombinu ya usafirishaji na mawasiliano kama vile reli na barabara, hivyo wizara na serikali kwa ujumla inadhamini na kulinda undugu huu wa kihistoria.” Alisema Jenerali Ibuge
Balozi Wang Ke ameshukuru kwa ushirikiano ambao amekuwa akiendelea kuupata kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Serikali kwa ujumla katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku.
Aidha, ameahidi kuendelea kutoa ushirikiano ili kuhakikisha serikali za nchi hizo mbili na watu wake wananufaika na uhusiano mzuri wa kidiplomasia uliopo.