Serikali imewakalibisha wawekezaji kutoka Dubai na mataifa mengine kote ulimwenguni kuwekeza katika sekta ya utalii nchini.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja amesema katika kongamano la uwekezaji sekta ya utalii linalofanyika leo Dis.15 mjini Dubai kwamba Tanzania ina fursa nyingi za uwekezaji katika maeneo ya mijini na sehemu mahsusi za utalii.
“Kuna umuhimu mkubwa kutumia fursa ya maonesho haya ya Expo 2020 Dubai kutangaza na kuelezea fursa za uwekezaji zilizopo nchini,” amesema Naibu Waziri akibainisha maeneo ya kiutamaduni na kihistoria, malazi kama hoteli za kitalii, migahawa, maeneo ya michezo ya gofi, utalii ikolojia, utalii wa kumbi za mikutano na utalii wa uwindaji.
Kongamano hili limehudhiriwa na Mkurugenzi wa Idara ya Uchumi ya Diplomasia Dubai, Balozi Edwin Rutageruka, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Allan Kijazi, Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Utalii nchini TTB, Betrita Lyimo, Bi. Hafsa Mbanga kutoka Kamisheni ya Utalii Zanzibar pamoja na Jumuiya ya Wafanyabiashara Dubai ikiwa ni sehemu ya Makongamano yaliyoandaliwa na Tanzania kwenye maonesho ya Expo 2020 Dubai.