Serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni mia tano (500) kwa ajili ya uzalishaji wa miche ya chai katika Wilaya ya Kilolo ambapo jumla ya miche milioni moja na laki tano itazalishwa na kuwanufaisha wakulima wa zao hilo katika Wilaya hiyo.
Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Chai Tanzania (TRIT) Dkt.Daniel Mgori amesema serikali imetoa fedha hizo ili kumrahisishia mkulima kupata miche ya chai kwa urahisi zaidi na kwamba miche hiyo itapelekwa kwa wakulima wa chai ndani ya Wilaya ya Kilolo.
Kwa upande wake Roda Chacha Mtafiti Msaidizi katika Taasisi ya Utafiti wa chai Tanzania anasema mpaka sasa tayari hatua mbali mbali za uzalishaji wa miche hiyo zinaendelea na wakulima watapata miche hiyo kwa wakati
Wakulima wa zao la chai Wilayani Kilolo wanaishukuru serikali kwa kufufua mashamba ambayo yalikuwa yametelekezwa na kuongeza kuwa kwa fedha zilizotolewa na serikali katika kuwasaidia wakulima kupata miche wanaimani watalima kilimo cha chai chenye tija kwao