Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Serikali yatangaza neema kwa wakulima wa mahindi

6b1a42b6b0287c4ec2dcce65e93774b4 Serikali yatangaza neema kwa wakulima wa mahindi

Thu, 22 Jul 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

BEI ya mahindi kutoka kwa wakulima inatarajiwa kuongezeka baada ya serikali kuanza kununua mahindi ili kuwezesha bei kuongezeka, huku ikiingia mikataba na kampuni za nje ya nchi kununua mahindi nchini.

Kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), serikali imepanga kununua tani 165,000 za mahindi kwa bei itakayomwezesha mkulima kuendelea.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa NFRA, Milton Lupa jana aliwaeleza waandishi wa habari kuwa, mwaka huu wa fedha wamepanga kununua tani 165,000 za mahindi na kwamba serikali imeahidi kuwapatia fedha hivyo mwisho wa mwezi huu wanatarajia kuanza kununua mazao katika awamu ya kwanza.

Lupa alisema kiwango hicho kinatarajiwa kuongezeka iwapo kutakuwa na wakulima waliokosa masoko na kubaki na mazao yao.

Alisema NFRA ina uwezo wa kuhifadhi tani 291,000 kwa sasa baada ya kukamilika kwa ghala Babati, mkoani Manyara lenye uwezo wa kuhifadhi tani 40,000 na ifikapo Juni, mwakani watakuwa na uwezo wa kuhifadhi tani zaidi ya 500,000 baada ya kukamilika kwa maghala yanayojengwa.

Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB) imepanga kununua tani 298,000 za mahindi na mazao mengine ukiwamo mtama, mpunga, maharage na alizeti na watayauza Kenya na Sudan Kusini.

Mkurugenzi Mkuu wa CPB, Anslem Moshi alisema katika mwaka huu wa fedha 2021/2022, bodi hiyo imepanga kununua tani 298,000 za mahindi, licha ya mazao mengine kama vile mtama, mpunga, maharage na alizeti.

Alisema kiwango hicho kitanunuliwa kupitia mikataba miwili ya kuiuzia kampuni ya Grain Industries Ltd ya Mombasa, Kenya tani 144,000 kwa mwaka na tayari tani 1,000 zimesafirishwa, huku wakikamilisha mazungumzo kuiuzia WFP tani 50,000 za mahindi na wakikamilisha kufungua ghala mjini Nairobi, Kenya kwa kushirikiana na kampuni ya Kapari Limited ya Dar es salaam inayomilikiwa na rai wa Kenya ili kupeleka takribani tani 102,000.

Alisema viwanda vya CPB vya kusaga mahindi vya Arusha, Iringa na Dodoma vinahitaji tani 54,000 za mahindi kwa mwaka hivyo kufanya mahitaji ya uhakika ya mahindi kwa mwaka 2021/2022 kuwa tani 298,000 zenye wastani wa thamani ya Sh. Bilioni 149 kwa wastani wa bei ya Sh 500 kwa kilo yakiwa kwenye ghala za CPB.

Alisema licha ya mahindi, Bodi hiyo imepanga kununua tani 60,000 za mtama mweupe kwa ajili ya soko la Sudan ya Kusini na tani 12,000 za alizeti kwa ajili ya kiwanda chake cha Kizota, Dodoma.

Alisema kwa sasa wametenga vituo vya muda vya kununua mahindi na mkoa wa Katavi wilaya ya Mlele wamefungua vituo Majimoto, Kashishi, Manela, Mirumba, Mbede, Itura, Kibaoni, Kavuu, Usevya na Chamaland.

Alisema tayari tani 1,000 zimenunuliwa katika vituo hivyo na kazi inaendelea na vituo vingine vitafunguliwa katika wilaya ya Tanganyika. Alisema wamekuwa wakinunua kwa wastani wa Sh 280 kwa kilo moja, huku mkoa wa Ruvuma walianza kununua kupitia vituo vya Songea mjini, na Kigonsera ambapo tayari tani 810 zimenunuliwa kwa bei ya Sh 280 kwa kilo.

Katika wilaya ya Nkasi ununuzi ulianza kuanzia juzi kati ya Sh 250 hadi Sh 270 kwa kilo moja, mkoa wa Songwe na maeneo ya Sumbawanga tani 10,823 zimenunuliwa kupitia wafanyabiashara wa kati wanaonunua na kuiuzia CPB, Iringa tani 8,903 kwa bei ya Sh 430 kwa kilo na Dodoma tani 1,920 kwa bei ya 450 kwa kilo.

Kanda ya Kaskazini Mahindi yamenunuliwa katika mkoa Manyara kwa bei ya wastani wa Sh 450 hadi 485 kwa kilo na tayari tani zimenunuliwa 1,553, hivyo Bodi imeshatumia Sh bilioni 7.47 kununua jumla ya tani 14,948 kwa wastani wa Sh 500 kwa kilo moja.

Chanzo: www.habarileo.co.tz