Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Serikali yatafiti usafirishaji mabasi mwendokasi

43809 Pic+mwendokasi Serikali yatafiti usafirishaji mabasi mwendokasi

Tue, 26 Feb 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Baada ya mvutano katika uendeshaji, Wakala wa Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka (Dart), umesema umemtafuta mshauri elekezi anayefanya utafiti kuhusu namna bora itakayokuwa na masilahi kwa pande zote mbili kati ya Serikali na sekta binafsi (PPP) katika huduma hiyo.

Meneja Uhusiano wa Dart, William Gatambi ameiambia Mwananchi kuwa utafiti huo utakaokamilika Juni utasaidia kutoa suluhu ya kudumu ya changamoto zilizopo na kushauri kama kuna haja ya kumpata mtoa huduma mwingine.

Kwa sasa, huduma ya usafiri katika awamu ya kwanza ya mradi huo (BRT) inatolewa na kampuni ya Udart tangu mwaka 2016 ulipozinduliwa na Gatambi alisema “endapo Udart wataonekana hawana matatizo mengi wataruhusiwa kuendelea kutoa huduma.”

Alifafanua kuwa lengo la utafiti unaoendelea kufanywa ni kujiridhisha kama mtoa huduma mmoja aliyepo katika awamu ya kwanza anatosha au kuna haja ya kuongeza ushindani kwa kuwa nao wengi zaidi.

Endapo itabidi, matokeo ya utafiti huo yataisaidia Dart kutangaza zabuni ya kumpata mtoa huduma mwingine, mpango huo utatekelezwa na Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango.

Kabla ya utafiti unaofanywa, Gatambi alisema kuna mtoa huduma mwingine alipatikana aliyekuwa akitumia miundombinu ya BRT, lakini aliondolewa baada ya kukiuka baadhi ya masharti ya mkataba.

Udart ilipewa leseni ya miaka miwili itoe huduma kuanzia mwaka 2016 mpaka 2018 kisha utaratibu mwingine ufuate. Wakati inapewa mkataba huo ilikuwa na mabasi 140 ingawa awamu ya kwanza inahitaji mabasi 305.

Ili kupunguza pengo lililopo, Udart iliagiza mabasi mengine 70 ambayo yamekwama bandarini baada ya kukosa kibali cha kuyaondoa kutokana na mvutano uliopo kati yake na Dart.

“Serikali imekusudia kuondoa mwanya wowote wa uvujaji wa mapato na kila upande unufaike,” alisema Gatambi.

Utakapokamilika utafiti unaoendelea, kama kutakuwa na sababu, alisema mtoa huduma mwingine atajulikana kati ya Julai na Agosti badala ya Machi kama ilivyopangwa.

Haya yote yanafanyika baada ya kipindi cha mpito kilichopewa Udart iliyoanza kutoa huduma Mei 2016 kukamilika kisha kuongezewa miezi sita mingine.

Kama mtoa huduma mwingine atapatikana, atalazimika kujazia mabasi yanayopungua (165) hivyo kuondoa kero iliyopo sasa ya abiria kusubiri kwa muda mrefu kituoni huku wakilazimika kusukumana kuwahi kuingia.

Awamu ya kwanza ya mradi huo inahudumia abiria wa kutoka Mbezi hadi Kivukoni huku kukiwa na mchepuko wa kwenda Gerezani, Morocco na Hospitali ya Taifa Muhimbili.



Chanzo: mwananchi.co.tz