Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Serikali yachuma bil 5/- kwa mwezi vinasaba vya mafuta

61fd523428d2a3e6fd6c3a5f74c2f341.jpeg Serikali yachuma bil 5/- kwa mwezi vinasaba vya mafuta

Thu, 10 Jun 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

SERIKALI inaingiza takriban Sh bilioni tano kwa mwezi kutokana na tozo ya vinasaba vinavyowekwa kwenye mafuta ya petroli na dizeli, kazi inayofanywa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS).

TBS ilianza kuweka vinasaba kwenye mafuta Aprili 28, mwaka huu kwa mafuta yanayotumika nchini na yasiyo na msamaha wa kodi.

Kabla ya TBS, kazi hiyo ilikuwa ikifanywa na Kampuni ya Global Fuel International (GFI) kwa kipindi cha miaka 10.

Akizungumza kwenye Jukwaa la Mafunzo kwa wahariri wa vyombo vya habari jana mkoani Dar es Salaam kuhusu majukumu ya TBS,

Mkuu wa Maabara ya Kemia wa TBS, Charles Batakanwa, alisema kwa mwezi serikali inapata kati ya Sh bilioni 4.6 hadi tano kutokana na tozo inayopatikana kwenye mafuta yenye vinasaba.

Kila lita moja ya mafuta inayouzwaihukatwa Sh 14 zinazoingia serikalini kama tozo ya vinasaba.

Kwa siku matumizi ya mafuta nchini ni kati ya lita milioni 12 hadi milioni 19 na takriban Sh milioni 154 hupatikana kwa siku kutokana na tozo hiyo ya vinasaba.

“Mafuta ambayo hatuyaweki vinasaba ni yale yaliyosamehewa kodi ambayo mara nyingi ni ya miradi mikubwa ya kimkakati ya serikali kama Bwawa la Kuzalisha Umeme la Julius Nyerere, SGR (Reli ya Kisasa) na mafuta yanayokwenda nje ya nchi,” alisema.

Aliabainisha faida ya kutumia taasisi ya serikali katika uwekaji wa vinasaba kwenye mafuta ni kuwapo uhakika wa usalama nchini, gharama nafuu na pia, taasisi ya serikali kuwa na uwezo mkubwa unaosaidia kudhibiti wakwepa kodi.

“TBS ina teknolojia ya kujua mafuta yaliyochanganywa na kitu kingine na kiwango cha asilimia yaliyokwepa kodi, yasiyo na ubora... Tunawawezesha EWURA (Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji) kutambua

mafuta yasiyokuwa na vinasaba katika vituo vyote vya mafuta,” alisema.

Huduma za vinasaba zinafanyika kwenye maghala yote ya mafuta yaliyopo nchini na idadi kwenye mabano ni Dar es Salaama (19), Mtwara (2) na Tanga (1).

Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dk Athumani Ngenya, alisema Ewura ilianza kuipa taarifa TBS ya kama inaweza kuweka vinasaba kwenye mafuta Februari mwaka huu ambapo TBS ilitaka ipewe miezi sita kujiweka sawa

kabla ya kuanza kazi hiyo.

“Tuliongea na Watanzania waliokuwa wanafanya kazi GFI na tukawachukua watusaidie, hivyo Aprili 28 (mwaka huu) tukaanza kuweka vinasaba baada ya kuona uwezo tunao,” alisema Ngenya.

Akizungumzia vipodozi vinavyotumika kwa ajili ya kujichubua ngozi, Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti Ubora wa TBS, Gervas Kaisi, alisema kikosi kazi kinachojumuisha polisi wa ndani, wa kimataifa

(Interpol), TCRA(Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania) na Usalama wa Taifa (TISS) kimefanikisha kukamata watu wengi wanaojihusisha na biashara ya vipodozi hivyo.

“Tayari wameshawafungulia kesi na zinaendelea, wengine wamelipishwa faini, TISS inatusaidia sana, hili ni endelevu... Hii biashara ni kama ya muuza bangi na mvuta bangi wanajuana wenyewe wanauziana vipi na wapi,”alisema.

Chanzo: www.habarileo.co.tz