Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Serikali yaanza mchakato viwanda vya simu janja

1ac0ccd8f49adef0d1d40a937eb4184a Serikali yaanza mchakato viwanda vya simu janja

Sun, 17 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

WIZARA ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari imeanza mchakato wa uanzishwaji wa viwanda vya utengenezaji wa simu janja ndani ya nchi vitakavyowezesha upatikanaji rahisi wa vifaa hiyo.

Waziri Dk Faustine Ndugulile alisema hayo jana wakati wa kikao kazi na wenyeviti wa bodi na wakuu wa taasisi zilizo chini ya wizara hiyo.

Alisema utaratibu umeshaanza na kiwanda kimojawapo kinatarajiwa kujengwa Mwanza wananchi wamudu kununua simu hizo nchini.

“Ilani ya CCM imetaka tuongeze wigo wa mawasiliano na kuongeza matumizi ya intaneti, hatutaweza kufanikiwa kama wananchi hawatamudu kununua simu janja. Na sisi tumeliona hilo na ndio maana tumeanza mchakato wa kuanzisha viwanda vyetu ndani ya nchi ambavyo vitaanza kutengeneza simu janja," alisema Dk Ndugulile.

Alisema kiwanda kitakachojengwa Mwanza kitakuwa kinazalisha simu na kuziunza kwa Watanzania kwa bei nafuu.

“Nitoe rai kwa Watanzania, mwekezaji yeyote mwenye nia ya kuwekeza kwenye Tehama aje kwenye wizara yetu na tutampa ushirikiano asilimia 100 kuhakikisha kwamba tunatengeneza bidhaa ambazo zitatumika ndani ya nchi ili wananchi wapate simu janja kwa gharama nafuu,” alisema.

Alisema duniani pamoja na kuwapo janga la corona kampuni zilizofanya vizuri na kupata faida kubwa zilikuwa ni za mitandao na kwamba Tanzania kwa sasa inapiga hatua.

“Tuna vijana wabunifu, hakodi fremu kwa ajili ya biashara anaagiza biashara yake nje ya nchi, anafikisha nchini anaweka nyumbani anapiga picha na kutangaza mitandaoni na anauza kupitia mtandao na kukufikishia mzigo wako nyumbani,” alisema.

Wakati huo huo, Dk Ndugulile aliwataka wenyeviti wa bodi na wakuu wa taasisi zilizo chini ya wizara hiyo kusimamia kudhibiti ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha na rasilimali za taasisi zao.

Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk Zainab Chaula alimhakikishia waziri kuwa aliyoagiza katika kikao kazi hicho yatatekelezwa kufikia maono ya Rais John Magufuli, ya kupanua wigo wa mawasiliano na matumizi ya intaneti.

Chanzo: habarileo.co.tz