Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Serikali yaandaa mkakati uchumi wa bahari

84f2708100b8ec3abe04749fd1efd49a.jpeg Serikali yaandaa mkakati uchumi wa bahari

Tue, 8 Jun 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

KATIKA mwaka wa fedha 2021/22, serikali imekuja vipaumbele kadha vilivyolenga kuziba mianya ya upotevu wa mapato, kulipa madeni na kutekeleza miradi ya maendeleo ikiwamo kuandaa Mkakati wa Kitaifa wa Uchumi wa Bahari.

Aidha, Bunge limepitisha makadirio ya mapato na matumizi kwa Wizara ya Fedha na Mipango ya Sh 12,961,271, 473,000. Kati ya fedha hizo, Sh 10,673,518,439,000 kwa ajili ya Deni la Taifa na huduma zingine. Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi pia imetengewa Sh 80,099,935,000.

Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2021/22, Waziri Dk Mwigulu Nchemba alisema vipaumbele viko kwenye maendeleo na vipaumbele vya kawaida.

Akifafanua upande wa matumizi ya maendeleo, Dk Mwigulu alisema wizara inatarajia kuandaa Mwongozo wa Usimamizi wa Mikataba, Ufuatiliaji na Tathmini, Usimamizi wa Vihatarishi vya Deni la Serikali pamoja na Vihatarishi vya Ununuzi wa Umma.

Alisema pia kuhuisha na kufungamanisha mifumo ya kielektroniki ya usimamizi wa fedha na mali za umma ili kudhibiti upotevu wa mapato na kuondoa matumizi yasiyo ya lazima na kurahisisha upatikanaji na usuluhishi wa taarifa za fedha.

Dk Mwigulu alisema kuandaa Mkakati wa Kitaifa wa Uchumi wa Bahari na kuwajengea uwezo watumishi kutoka wizara, idara zinazojitegemea, wakala za serikali, taasisi na mashirika ya umma, mikoa na mamlaka za Serikali za Mitaa kuhusu matumizi ya mifumo ya usimamizi na udhibiti wa mapato, matumizi na mali za serikali;

Alisema pia kuimarisha usalama na ulinzi wa mifumo ya Tehama pamoja na mifumo ya usimamizi na udhibiti wa mapato, matumizi na mali za serikali na kuendelea na ujenzi wa jengo la wizara katika Mji wa Magufuli pamoja na Jengo la Ofisi ya Usimamizi wa Mali za Serikali mkoani Geita.

Kwa upande wa vipaumbele vya matumizi ya kawaida, Dk Mwigulu alisema wizara inatarajia kufanya mapitio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, Mpango Elekezi wa Miaka 15 (2011/12 – 2025/26) na kuanza maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kufanya tafiti za kiuchumi na modeli za fedha ili kubaini fursa fiche za uwekezaji na vyanzo vipya vya mapato, ikiwa ni pamoja na mapato ya kugharamia shughuli za Muungano.

Pia kufanya tathmini ya kina ya mfumo wa mapato na matumizi ya serikali ili kubaini maeneo yenye upungufu au changamoto na kupendekeza hatua stahiki za kuchukua na kufanya tathmini ya Uhimilivu wa deni la Serikali (DSA).

Alisema pia kuratibu mipango na mikakati ya upatikanaji wa misaada, mikopo yenye masharti nafuu na mikopo yenye masharti ya kibiashara kwa ajili ya kugharamia bajeti ya Serikali na kutunga Sera ya Maendeleo ya Sekta ya Benki na Mkakati wake.

Alikitaja kipaumbele kingine kuwa ni kuhuisha Mpango Mkakati wa Wizara wa Miaka Mitano (2022/23 - 2026/27).

Pia kuandaa Mwongozo wa Usimamizi, Tathmini na Ufuatiliaji wa Uwekezaji katika Taasisi na Mashirika ya Umma, kufanya ufuatiliaji, tathmini, ukaguzi, udhibiti na uhakiki wa mapato, matumizi, miradi ya maendeleo, mali za umma; na miamala ya utakasishaji wa fedha haramu na ufadhili wa ugaidi.

Alisema pia kuandaa Mkakati wa Utekelezaji wa Sera ya Ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP), kukamilisha maandalizi ya Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo na kufanya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 na Kutunga Sera ya Taifa ya Idadi ya Watu na Mkakati wa utekelezaji wake.

Chanzo: www.habarileo.co.tz