Tabora. Serikali ya Tanzania imeahidi kufanya udhibiti wa dawa feki za kuulia wadudu katika zao la pamba kwa lengo la kuwanusuru wakulima wasipate hasara.
Akizungumza na wakazi wa kijiji cha Mwabakima leo Jumatatu Julai 15, 2019 Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema Serikali inafahamu kuna dawa feki zinauzwa na wakulima wanazinunua ambazo haziwasaidii kwa vile haziuwi wadudu.
Amesema kutokana na hali hiyo, Serikali italisimamia eneo hilo kwa lengo la kuwalinda wakulima wasinunue dawa isiyowasaidia.
"Nawaomba wakulima suala hili mliachie Serikali iweze kudhibiti hali hiyo," amesema
Amewahakikishia wakulima wa pamba kuwa Serikali itahakikisha dawa zinazotumika ziwe ni zile zinazoua wadudu na sio vinginevyo na kwamba haitawaangusha wakulima hao.
Ameeleza wameimarisha Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na kuimarisha chuo cha Ukiriguru na kuwaondoa wasiwasi kuwa hali itakuwa nzuri.