Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Serikali ya Tanzania yaionya Halotel

78901 Halotel+pic

Mon, 7 Oct 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano nchini Tanzania, Atashasta Nditiye ameionya kampuni ya simu ya Halotel nchini kuacha kutumia mkongo wa Taifa wa mawasiliano kupeleka mawasiliano nje ya nchi.

Nditiye ametoa kauli baada ya kubaini kampuni hiyo  inapeleka mawasiliano yake kutoka Tanzania kwenda Burundi kwa kuunganisha jozi za mawasiliano za kampuni hiyo kwenye mfumo wa mkongo wa Burundi badala ya kufanya maunganisho huo kupitia Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano (Nictbb).

Nditiye ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Oktoba 7,2019  katika ziara ya  kukagua miundombinu na mwingiliano wa mawasiliano kati ya  Kabanga mpakani mwa Tanzania na Burundi.

Nditiye ametoa kauli hiyo baada ya kufika katika maunganisho ya mkongo wa Taifa wa mawasiliano  unaotumika kupeleka mawasiliano kutoka Tanzania kwenda nchi jirani.

“Nawaelekeza Halotel watumie mkongo wa Taifa wa mawasiliano kupeleka mawasiliano nchi jirani ili kufuata utaratibu uliowekwa baina ya nchi moja na nyingine wa kuvusha mawasiliano yake kwenda nchi jirani,” amesema  Nditiye.

Nditiye amesema  Halotel hawaruhusiwi kufanya hivyo, akibainisha kuwa wanakiuka utaratibu na  wanaikosesha nchi mapato sambamba kuhatarisha usalama  wa Taifa kwa kuwa hakuna atakayeweza kufuatilia mawasiliano upande wa pili wa nchi hiyo.

Pia Soma

Advertisement
Mhandisi wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Marwa Mwita amesema ameyapokea maelekezo ya Nditiye na kukiri kuwa hakuna kampuni ya mawasiliano ya simu ya mkononi inayoruhusiwa kuvusha mawasiliano kutoka nchi moja kwenda nchi nyingine bila kupitia Mkongo wa Taifa wa nchi husika.

Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Kanali Michael Mntenjele amesema  wilaya inahitaji mawasiliano ya uhakika na yasiyokuwa na msongamano ili kufanikisha suala la ulinzi na Usalama wa Taifa.

Chanzo: mwananchi.co.tz