Dar es Salaam. Serikali na wadau wa kilimo wameanza kupitia rasimu ya kwanza ya sheria ya matumizi bora ya zana za kilimo lengo ikiwa kuwabana waingizaji wa bidhaa feki.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Methew Mtigumwe leo Jumatatu Desemba 3, 2018, amesema lengo la kufanya hivyo ni kuwapunguzia usumbufu wakulima wanaouziwa zana ambazo hazikidhi ubora.
“Tumekutana hapa kujadiliana sheria mbalimbali zitakazoweza kuwabana waingizaji na wasambazaji wa zana ambazo hazina ubora na sheria hiyo itaanza kutumika miezi sita ijayo,” amesema Mtigumwe.
Amesema nchi ipo katika uchumi wa viwanda kwa sasa lazima kuwe na udhibiti utakaoleta tija kwa wakulima na kuwafanya wao wapate faida badala ya hasara.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa zana za kilimo na Umwagiliaji, Joseph Lubiloh amesema ili nchi iwe na viwanda, uzalishaji unapitia katika sekta ya kilimo.
Amesema ni vema dhana zikawa bora na endelevu katika kumsaidia mkulima.
Lubiloh amesema sheria hiyo itasaidia kuwabana wauzaji, wasambazaji na kuwasaidia watumiaji kwa kuwa watakuwa na uhakika wa uzalishaji pia.
KIwa sasa amesema Serikali inatoa mazingira wezeshi kwa kupitia vyama vyao kuwakopesha wakulima pembejeo zitakazowasaidia kuwakwamua kiuchumi.
Kwa upande wa wasambazaji, Meneja Yahya Sagati kutoka kampuni ya MeTL Agriculture amesema sheria hiyo ikisimamiwa na kutekelezwa itawasaidia wakulima hata kudhibiti wauzaji wa zana feki.