Serikali imeahidi kudhibiti vitendo vya uvamizi kwa wavuvi ndani ya ziwa Victoria linalopelekea wavuvi kupoteza mali zao na kuuawa.
Kauli hiyo imetolewa leo Ijumaa Machi 4, 2022 na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdalah Ulega alipokuwa akizunguma na wavuvi mkoani Musoma.
Ulega amesema Serikali imefikia hatua hiyo baada ya kuwepo kwa malalamiko mengi juu ya vitendo hivyo vya uvamizi, ingawa waziri hakutoa takwmimu juu ya vitendo hivyo hasa katika maneneo ya mipakani huku watuhumiwa wakidaiwa kutoka nchi za jirani.
"Kuna vitendo vingi vya uvamizi wanafanyiwa wavuvi wetu na wahusika inasemekana wanatoka nje ya nchi kwa hiyo wizara yetu pamoja na wizara ya mambo ya ndani hivi sasa tuko katika majadiliano juu ya namna ya kukomesha vitendo hivyo na muda si mrefu tutakuja na mwarobani wa tatizo hili.
"Matukio haya yanapelekea wavuvi wetu kupoteza mali zao, mitaji na hata kuhatarisha maisha yao hivyo wizara yetu imepokea suala hili na tunalifanyia kazi kwa kushirikiana na wenzetu wa mambo ya ndani na muda si mrefu tutapata muafaka" amesema Ulega
Akizungumzia vitendo hivyo Mwenyekiti wa wamiliki vyombo vya uvuvi katika Mwalo wa Makoko, Joseph Chata amesema vitendo vya uvamizi ndani ya ziwa Victoria vimekuwa vikitokea mara kwa mara huku walengwa wakuu wakiwa ni wavuvi wa Tanzania.
Advertisement "Vitendo hivi mara nyingi vinafanyika hasa kwenye maeneo ya mipakani na wavamizi wanatoka nje ya nchi na vimekuwa vikiwaathiri wavuvi sana na mbaya zaidi vinatokea maeneo ambayo hakuna mtandao na wakivamia wanachukua kila kitu kuanzia chombo hadi samaki kisha wanakuacha unaelea huko ziwani" amesema