Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Serikali kukomaa na wanaotoroshea nje madini

56745 PIC+MADINI

Mon, 13 May 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Mwanza. Huku uamuzi wa kufungua masoko rasmi ya madini ukionyesha mauzo yameanza kuongezeka, Serikali imetangaza kuwashughulikia watu watakaojaribu kuyatorosha nchini ikisema licha ya kufungwa jela, watakuwa maskini kwa mali zao kufilisiwa.

Kwa mujibu wa katibu mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila, masoko 17 yameshafunguliwa katika maeneo ya Geita, Kahama, Shinyanga, Namanga mkoani Arusha, Singida, Chunya, Ruvuma, Katavi, Dodoma, Kigoma, Tabora, Mara, Kagera, Mbeya, Mwanza, Iringa na Songwe.

Mpaka mwishoni mwa mwezi huu, masoko mengine yatakuwa yamefunguliwa Tanga, Mbulu na Babati mkoani Manyara, Kilimanjaro, Morogoro, Handeni, Lindi, Simiyu na Rukwa.

Akizindua Soko la Kimataifa la Madini mkoani Mwanza, Waziri wa Madini, Dotto Biteko alisema juzi kuwa, “nawatahadharisha wachimbaji na wafanyabiashara waache kutorosha madini nje ya nchi kwa sababu kufanya hivyo ni kujiweka kwenye hatari ya kugeuka maskini kwa mali zao kutaifishwa pamoja na kufungwa jela.”

Akizungumza mbele ya wafanyabiashara wadogo, kati na wakubwa wa madini, viongozi wa dini na watendaji wa Serikali, Biteko alisema Serikali itaendelea kutumia sheria, kanuni na taratibu kuziba mianya yote iliyokuwa ikitumiwa na watu wasio waaminifu kutoroshea madini nje ya nchi na kuikosesha Taifa mapato. “Hatutarudia makosa yaliyosababisha baadhi ya mataifa kujizolea sifa ya kuongoza kwenye soko la dunia kwa kuuza madini yanayopatikana Tanzania pekee.”

Machi 28, akizungumza na wanahabari jijini Mwanza, mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Biswalo Mganga alisema Serikali imetaifisha kilo 343 za dhahabu katika matukio tofauti yaliyohusiana na uvunjifu wa sheria kati ya Aprili, 2018 hadi sasa.

Pia Soma

Kuhusu masoko rasmi ya madini, Waziri Biteko alisema Geita na Chunya yameonyesha mafanikio baada ya mauzo kuongezeka maradufu akisema lile la Geita linarekodi kilo 198 kwa mwezi tangu lizinduliwe huku Chunya likishuhudia kilo 22 za dhahabu zenye thamani ya zaidi ya Sh1.8 bilioni ndani ya siku nne tangu lifunguliwe.

Pamoja na kupongeza uamuzi wa kufungua masoko rasmi, mfanyabiashara wa madini mkoani Mwanza, Makona Kaniki aliiomba Serikali kuhakikisha yanakuwa na watumishi wa kutosha kulingana na mahitaji ili kuwaondolea wafanyabiashara adha ya kutumia muda mrefu kupata huduma.

Chanzo: mwananchi.co.tz