SERIKALI imeziomba sekta binafsi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika uwekezaji wa ujenzi wa reli ambayo inatarajiwa kujengwa katika ushoroba wa Mtwara kuunganisha Bandari ya Mtwara na Mbamba-Bay na matawi yake ya Liganga na Mchuchuma.
Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi Profesa Godius Kahyrara katika mkutano wa wadau kuhusu maendeleo ya ushoraba ulioandaliwa na Mamlaka ya Usimamizi Bandari Tanzania (TPA) mkoani Mtwara.
Katika hotuba yake iliyosomwa na Devota Gabriel ambaye ni Mkurungezi wa Ufuatiliaji na Tathmini katika Wizara ya Uchukuzi, Profesa Kahyrara, amesema serikali iko tayari kutoa ushirikiano wa kutosha, ili kuhakikisha mazingira ya biashara yanakuwa rafiki na yanayovutia ili uwekezaji utakaofanyika kuwa wenye matokeo chanya kwa wawekezaji.
"Tunatambua umuhimu wa ushirikiano baina ya serikali, sekta binafsi, wadau wa maendeleo, na jamii nzima katika kufanikisha malengo yetu. Hivyo basi, napenda kuwahimiza nyote mshiriki kikamilifu katika majadiliano ya leo kwa kuleta mawazo na mapendekezo yenu yenye tija, "amesema.