TAASISI ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) inatarajiwa kushiriki kwenye kongamano la siku moja mkoani Songwe linalolenga kuwaeleza vijana fursa za kiuchumi mkoani mwao na Tanzania kwa jumla hapo kesho.
Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF, Godfrey Simbeye, alisema jana jijini Dar es Salaam kuwa moja ya shabaha kuu za TPSF ni kuhakikisha sekta binafsi ya siku za baadaye inajengwa na vijana wabunifu, wanye kujituma sana na wenye kufanyakazi zenye tija.
“Kama sehemu ya mikakati yetu ya miaka mitano, TPSF kwa kushirikiana na wenzetu wa Mkoa wa Songwe, tumeandaa kongamano la vijana ambalo litafanyika Jumamosi ijayo. Katika kongamano hilo fursa mbalimbali zitaonyeshwa na namna vijana wanavyoweza kuwa sehemu muhimu katika ukuaji wa sekta isiyo rasmi hapa nchini,” alisema Simbeye.
Ametoa wito kwa vijana wa Mkoa wa Songwe kuhudhuria kongamono hilo ili kupata ufafanuzi na maelezo juu ya fursa zilizomo mkoani mwao na ambazo zitawasaidia vijana kujikwamua kiuchumi.