Mrajisi wa Vyama vya Ushirika, Dk Benson Ndiege amewaagiza viongozi wa vyama vya ushirika wa akiba na mikopo nchini (Saccos) wafunge hesabu za mwaka 2021 na kuziwasilisha kwa wakaguzi wa nje.
Dk Ndiege ambaye pia ni Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), alitoa agizo hilo kupitia taarifa aliyoituma jana kwa vyombo vya habari.
Alisema mwaka wa fedha wa saccos unaanzia Januari Mosi na kuisha Desemba 31 kila mwaka na kwamba muda umepita na saccos zinapaswa kufunga hesabu.
Hiyo alisema ni kwa kuzingatia matakwa ya kifungu cha 55 (2) cha sheria ya vyama vya ushirika namba 6 ya mwaka 2013 na kanuni ya 55 ya vyama vya ushirika ya mwaka 2015.
Alisema Saccos zinapaswa kuwasilisha taarifa hizo kwa Mkaguzi wa Nje ambaye ni Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (Coasco) ili zikaguliwe.
Katika taarifa hiyo alisema viongozi wa Saccos wanapaswa kujibu hoja zote zilizotolewa na zitakazotolewa na wakaguzi ili kuondokana na uwepo wa hati zisizoridhisha pamoja na hati chafu.
"Chama kitakachoshindwa kujibu hoja husika na kupata hati chafu, viongozi na watendaji wake watapaswa kuwajibika kwa kuzingatia matakwa ya Kifungu cha 55(13) cha Sheria ya Vyama vya Ushirika, kanuni ya 85(g) ya Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha (SACCOS) za Mwaka 2019," alisema.