MFANYABIASHARA maarufu nchini Tanzania, Rostam Aziz amesema Kenya imekuwa ikiwapa vikwazo wanapotaka kuwekeza nchini humo hivyo kukwaza ushirikiano wa kibiashara kwa watu wa mataifa hayo mawili.
Aliyasema hayo jana jijini Nairobi alipozungumza kwenye jukwaa la wafanyabiashara wa Kenya na Tanzania.
Rostam alisema ni rahisi kwa Wakenya kuwekeza nchini Tanzania kuliko Watanzania kuwekeza nchini humo.
Alitoa mfano akisema kwa zaidi ya miaka mitatu amezungushwa na mamlaka za Kenya kuwekeza mradi wa gesi nchini humo jambo linaloonesha kuwa Wakenya wananufaika zaidi nchini Tanzania kuliko Watanzania wanapotaka kuwekeza Kenya.
“Ndugu, uwekezaji huu ni mkubwa, si wa nyanya…Tanzania na Kenya kiuwezo zinaweza kuwa kubwa zaidi ya zilivyo sasa, lakini kwa bahati mbaya tumeushusha kwa siasa, kutokuwa na uhakika wa usalama, ushirikiano usio mzuri unahatarisha uchumi wa nchi zetu,” alisema Rostam.
Rostam alisema uhusiano wa kibiashara baina ya Tanzania na Kenya una faida kwa upande mmoja zaidi na ili kudhihirisha hilo, kuna kampuni zaidi ya 500 za Kenya zimewekeza nchini Tanzania lakini kampuni 30 tu za Tanzania zimewekeza Kenya.
“Watanzania tumejaribu kuja kuwekeza Kenya lakini kumekuwa na vikwazo. Mimi tangu mwaka 2017 nilikuja hapa, nikakutana na Rais Uhuru Ikulu, akanikaribisha nije niwekeze Kenya, akaniuliza niwekeze nini, nikamwambia naona kuna fursa ya gesi. Lakini ilinichukua three years (miaka mitatu) nazungushwa tu na mpaka sasa zijapata majibu,” alilalamika Rostam.