Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Rais Samia awataka wananchi kuwapisha wawekezaji

Rais Samia Awataka Wananchi Kuwapisha Wawekezaji.jpeg Rais Samia awataka wananchi kuwapisha wawekezaji

Tue, 17 Oct 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewataka wananchi mkoani Singida kuwapisha wawekezaji wanapokuja kwa ajili ya kuwekeza katika Rasilimali Madini mkoani humo.

Amesema hayo leo Oktoba 16, 2023 katika uwanja wa Bombadia, Singida Mjini wakati akihutubia katika Maadhimisho ya Miaka 60 ya mkoa wa huo.

“Tuna madini Singida, yakiwemo Dhahabu, Urania, Shaba, Jasi, Chumvi, Shumalin, Virkulu, Lithium chungu nzima yote haya yapo Singida, sasa wanapokuja wawekezaji tusiwe majoka ya mdimu, tuwapishe watumie maeneo waijenge Singida, wapate faida yao walikuja kufanyia kazi." amesema Dkt. Samia.

Kwa upande wake, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amesema kuwa Serikali itawapatia leseni Wachimbaji Wadogo wa Madini katika eneo la Muintiri, wilayani Ikungi mkoani Singida ili kuendesha shughuli zao za uchimbaji bila usumbufu.

Amesema kwa kuwa mkoa wa Singida ni moja ya mikoa iliyojaaliwa kuwa na Rasilimali Madini hivyo ili kuongeza Mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa na uchumi kwa ujumla, Serikali imeamua kutoa leseni kwa Wachimbaji Wadogo ili wachimbe madini katika mkoa Singida.

Aidha, katika kuendelea kuboresha shughuli za uzalishaji kwa wachimbaji wadogo, Waziri Mavunde amesisitiza kuwa Oktoba 21, 2023, jijini Dodoma Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya kukabidhi mitambo mitano ya uchorongaji kwa Wachimbaji Wadogo, mitambo hiyo imenunuliwa na Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO).

Akizungumzia mafanikio ya Sekta ya Madini katika mkoa wa Singida, Mhe. Mavunde amesema mgodi wa Singida Gold Mine unaomilikiwa na Kampuni ya Shanta Mine ambao umeanza uzalishaji mwezi machi 2023, tayari umezalisha kilogramu 400 za Dhahabu ikiwa ni hatua kubwa katika sekta ya madini katika mkoa huo.

Sambamba na hilo, Waziri Mavunde amesema kuwa Serikali iko mbioni kukamilisha skimu ya umwagiliaji katika kata ya Mang’onyi wilayani Ikungi kwa ajili ya wakulima kulima mwaka mzima na kwamba kupitia Ushirika ya Mang’onyi wameshazungumza na mgodi huo wa Dhahabu wa Singida na tayari umekubali kununua mazao yatakayozalishwa hapo na wakulima wa Ikungi na Singida kwa ujumla.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live