Dar es Salaam. Rais John Magufuli ameahidi kutoa Sh20 milioni kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa ofisi ya wajasiriamali katika soko la Feri jijini Dar es Salaam.
Pia, ameahidi kuzifanyia kazi changamoto mbalimbali zinazowakabili wajasiriamali hao katika shughuli zao.
Taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Oktoba Mosi, 2018 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa inaeleza kuwa Rais Magufuli amekutana na wajasiriamali hao akiwa katika mazoezi ya jioni pamoja na mkewe, Janeth aliyewachangia wajasiriamali wanawake Sh5 milioni.
Wajasiriamali hao walimuomba Rais Magufuli kuwasaidia wasifukuzwe na manispaa ya Ilala katika eneo hilo badala yake wawekewe utaratibu mzuri wa kufanya biashara zao.
Pia, wamemuomba Rais Magufuli waondolewe ushuru unaotozwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri na Maji na Nchi Kavu (Sumatra) kwa mitumbwi ya wavuvi wadogo wa samaki kama ambavyo Serikali ilivyowaondolea ushuru wakulima wanapopeleka sokoni mazao yasiyozidi tani moja.
Rais Magufuli ameahidi kufanyia kazi maombi hayona amewapongeza kwa juhudi zao za kujitafutia kipato.