Mkuu wa Mkoa wa Mara, Ally Hapi ameiagiza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani humo kuwa wabunifu na kuweza kufikisha elimu ya ulipaji kodi kwa wafanyabiashara.
Hapi ameitaka taasisi hiyo kupanua wigo wa ukusanyaji wake wa mapato hususani vijijini.
Hapi ameyatoa maagizo hayo mjini Musoma kwenye kikao chake na wadau wa kodi mkoani humo ambapo pamoja na mambo mengine washiriki wa kikao hicho wamesema kuwa wafanyabiashara wengi hawana elimu juu ya ulipaji kodi hivyo wengi wao hufanya biashara kwa mazoea tu.
"Mmewasikia wafanyabiashara wengi hawana elimu ya ulipaji kodi wao wanaendesha biashara zao kwa mazoea na wana mapesa mengi pamoja na kwamba baadhi yao ni wale wa darasa la saba ni jukumu lenu kukaa nao kuwapa elimu, wengi wanakuwa na hofu kutokana na habari za mitaani lakini mkiwafiikia na kuwapa elimu nina uhakika wote watakuwa walipa kodi wazuri tena kwa hiari" amesema
Ameongeza kuwa mamlaka hiyo pia inatakiwa kuyaangalia makundi ya wafanyabishara wadogo hasa waliopo vijijini ili kuwatengenezea mazingira mazuri ya biashara.
" Kule kuna wafanyabiashara wenye sifa hakuna tu utaratibu maalum uliowekwa ili kuwatambua na matokeo yake mzigo wa kulipa kodi upo kwa watu wachache fikeni kule ongeeni nao wapeni elimu tengenezeni urafiki nao na mtaongeza idadi ya walipa kodi " amesema
Akizungumza kwenye kikao hicho mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara wa Kilimo na Viwanda (Tccia) mkoani humo, Boniphace Ndengo amesema mbali na ukosefu wa elimu lakini pia wingi wa tozo za serikali na taasisi zake kwa wafanyabiashara ni sababu nyingine inayoplekea wafanyabiashara kukwepa kodi.
Meneje wa TRA mkoaani humo, Adam Ntoga amesema Mamlaka hiyo imekuwa na desturi ya kukutana na wafanyabiashara kujadiliana ili kudumisha mahusiano baina ya taasisi hiyo na walipa kodi.