Dar es Salaam. Pundamilia wa tofauti ambaye hivi karibuni alionekana katika mbuga ya wanyama ya Maasai Mara nchini Kenya ameingia katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti iliyoko mkoani Mara nchini Tanzania.
Pundamilia huyo ambaye ana vidoti vidoti na rangi nyeusi tofauti na pundamilia wengine amevuka mpaka na kuingia Serengeti akiwa na pundamilia wengine na nyumbu ambao walikuwa wanahama.
Pundamilia huyo anakuwa wa pekee tofauti na pundamilia wengine kwa kuwa yeye ana madoadoa meupe na mistari michache myeupe tofauti na wengine ambao wanakuwa na mistari myeupe kwenye ngozi.
Pundamilia huyo ambaye alionekana kwa siku za hivi karibuni katika hifadhi ya taifa ya Maasai Mara nchini Kenya anakadiriwa kuwa na mwezi mmoja.
Baadhi ya watalii na waongoza watalii wamesema wamemuona mnyama huyo akivuka kwenye mto ambao unatenganisha hifadhi ya Maasai Mara kwa upande wa Kenya na Serengeti ya Tanzania.
Taarifa kutoka kwa kiongozi wa waongoza watalii na katibu wa chama cha madereva wa watalii nchini Kenya, Felix Migoya zinasema kuwa kwa sasa pundamilia huyo ambaye ana umri wa mwezi mmoja yupo kaskazini mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Pia Soma
- Mrembo Gigi avaana na aliyevamia jukwaa la Fashion Show
- Harmonize kuiwakilisha Afrika Mashariki tuzo za MTV Europe Music Awards 2019
- Waziri Bashungwa akerwa na utendaji wa kiwanda cha Nyuzi Tabora
- Wamiliki kiwanda cha Nyuzi walalamikia ukosefu wa masoko