Prof. Mkumbo ameyazungumza jana alipotembelea TanTrade na kukagua matayarisho ya Maonesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanayotarajia kuanza Juni 28 hadi Julai 13, 2021 katika Uwanja wa Maonesho wa Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, Dar es Salaam.
Alisema kuwa lengo la maonesho ya mwaka huu ni kutoa fursa kwa Wafanyabiashara wa ndani na nje ya nchi pamoja na taasisi mbalimbali kutangaza biashara, bidhaa na huduma, kujifunza masuala ya biashara na teknolojia bora za uzalishaji wa bidhaa kulingana na soko la kimataifa, kutengeneza mitandao ya mawasiliano itayowasaidia kukuza biashara na kupata wabia wa biashara ili kufikia malengo waliyojiwekea.
Aidha, ameridhishwa na kasi ya maandalizi ya Maonesho ya mwaka huu na kuwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kutembelea maonesho ya mwaka huu yenye kauli mbiu isemayo 'Uchumi wa Viwanda kwa Ajira na Biashara Endelevu'.